• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Hazina za wanawake, vijana kuunganishwa

Hazina za wanawake, vijana kuunganishwa

Na SIAGO CECE

Serikali itaunganisha hazina tatu za Uwezo, Wanawake na Vijana kuwa moja na kuongezea pesa hazina mpya itakayobuniwa kwa lengo la kufanya watu wengi kuchukua mikopo ambayo itakuwa na riba ya chini.

Waziri wa Fedha, Ukur Yatani, alisema kwamba wanabadilisha kanuni kadhaa, ya kwanza ikiwa kubuni Hazina ya Biashara ambayo itanufaisha wamiliki wa biashara ndogo.

Bw Yatani alisema kwamba serikali, kupitia hatua hiyo, itaongeza pesa za Hazina ya Biashara kutoka Sh2.4 bilioni hadi Sh14 bilioni.

“Kupitia Hazina ya Biashara, serikali itapunguza gharama kwa kupunguza idadi ya wafanyakazi na hazina itakua zaidi ya mara sita,” Yatani aliambia kamati ya bunge inayokutana Mombasa.

Aliongeza: “Tuko katika hatua za mwisho za kuunganisha hazina hizo ili kuziimarisha ziweze kuafikia malengo yake ya kutoa mikopo na kuondoa changamoto kama gharama ya kuziendesha,” alisema.

Kamati inayosimamiwa na mbunge wa Tiaty, William Kamket inaendelea kutoa mapendekezo kuhusu hazina hiyo ambayo Bw Yatani alisema yanamfurahisha.

“Tunachunguza sheria kadhaa na ya kwanza ni kubuniwa kwa Hazina ya Biashara. Tunataka kuimarisha mfumo wote,” alisema na kukiri kulikuwa na visiki awali.

Alisema miongoni mwa masuala wanayotaka kutatua ni pamoja na kuwa na maafisa wa hazina za vijana, wanawake na Uwezo katika miji mingi kote nchini wanaohudumu kivyao jambo linalofanya gharama kuwa kubwa.

Bw Yatani alisema kwamba wanataka kuhakikisha kuwa vyama vya akiba na mikopo na vyama vingine vinapatiwa nafasi ya kwanza kupata pesa hizo ili vijiimarishe.

Mnamo Agosti 2019, serikali ilisimamisha shirika lililokuwa likitoa mikopo kwa wanawake, vijana na biashara ndogo kwa riba ya asilimia sita.

Katika ripoti, kamati ya bunge kuhusu majukumu maalum ilisema kwamba sheria ya Hazina ya Biashara ya 2019 inakiuka Katiba na hivyo ikapendekeza ibadilishwe yote.

Kamati hiyo ilisema kwamba umma haukushirikishwa kikamilifu na hazina hiyo ingebuniwa kupitia sheria mpya wala si kubadilishwa kwa sheria iliyokuwepo.

Lakini Bw Yatani alisema Hazina ya Biashara inafaa kuanzishwa wakati huu kwa sababu tayari wamepata mafunzo kutoka hazina zilizotangulia na kutambua kuwa kulikuwa na shida.

Alisema itafaa zaidi kwa kuwa serikali itapunguza gharama na kuweka mikakati ili iweze kunufaisha watu wengi. Hazina hizo zilianzishwa na serikali kusaidia vijana na wanawake kuanzisha bishara kama mkakati wa kukabiliana na ukosefu wa ajira.

You can share this post!

Masaibu ya Sonko yazidi huku kesi zikifufuliwa

GWIJI WA WIKI: Tabitha Manzi