• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:50 AM
Raila asema Ruto aliarifiwa kuhusu handisheki na Rais

Raila asema Ruto aliarifiwa kuhusu handisheki na Rais

Na SAMMY WAWERU

Naibu wa Rais Bw William Ruto alifahamishwa kuhusu salamu za maridhiano (Handisheki) kati yangu na Rais Uhuru Kenyatta, amesisitiza kiongozi wa ODM Raila Odinga.

Bw Odinga amesema baada ya mashauriano kati yake na Rais Kenyatta kuzika tofauti zao za kisiasa, kufuatia mgawanyiko ulioshuhudiwa katika uchaguzi mkuu wa 2013 na 2017, Rais alimuarifu naibu wake kuhusu mipango itakayojiri.

“Alipigia makamu wake simu nikiwa, akamwambia ‘ukiona mimi na Raila tunatoa taarifa usiwe na wasiwasi, nitakueleza mengi baadaye’…” akadokeza.

Kiongozi huyo wa upinzani pia amesema aliarifu mgombea mwenza, Bw Kalonzo Musyoka (Wiper) kuhusu matazamio ya salamu za maridhiano.

Rais Kenyatta na Bw Odinga walihutubia taifa mnamo Machi 9, 2018, wakiahidi kuzika tofauti zao za kisiasa ambapo pia walizindua Ripoti ya Mpango wa Maridhiano, BBI.

Akionekana kumsuta Naibu wa Rais William Ruto kufuatia madai yake kuwa hakuhusishwa katika hatua hiyo, Raila alisema Dkt Ruto pia alishirikishwa kuteua wanachama wa jopokazi la BBI lililobuniwa kukusanya maoni ya umma, katika mchakato mzima kuunganisha taifa.

Aidha, jopokazi hilo lina wanachama 14. “Kati ya wanachama hao, Rais aliwakilishwa na wataalamu saba, nami pia saba. Kati ya saba wa Rais, watatu walipendekezwa na Ruto,” Bw Odinga akafafanua.

Jopokazi hilo lilijukumika kukusanya maoni mseto ya Wakenya, kilele kikiwa mapendekezo ya Katiba kufanyiwa marekebisho kupitia BBI.

“Si haki kusema makamu wa rais alikuwa kwa giza, alikuwa ndani na hakushurutishwa na yeyote. Alielezwa atoe maoni yake kuhusu BBI ila hakutoa, watu wake ndio walitoa. Walikuwa wakimshauri na kumweleza yaliyojiri,” akaelezea.

Bw Odinga ametetea jopokazi la BBI, akihoji lilikuwa huru katika ukusanyaji wa maoni na uandaaji wa Ripoti ya Maridhiano.

Aidha, Dkt Ruto amenukuliwa hadharani akikosoa uhalisia wa BBI na Handisheki. Wandani wake wanadai salamu za maridhiano zililenga kuzima ndoto zake kuingia Ikulu 2022.

You can share this post!

Mswada wa Kura ya Maamuzi kupewa kipaumbele bungeni

THIS LOVE: Wakenya wawapongeza Nameless na Wahu kwa utunzi...