• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 12:58 PM
Joho, Kingi mbioni kufufua jumuiya ya Pwani

Joho, Kingi mbioni kufufua jumuiya ya Pwani

Na LUCY MKANYIKA

MKUTANO wa faragha wa magavana wanne wa Pwani mnamo Jumatano unaonekana kuwa mojawapo ya mbinu za kuwapa uhai wa kisiasa magavana Hassan Ali Joho (Mombasa) na Amason Kingi (Kilifi).

Wawili hao ambao sheria inawazuia kuwania ugavana kwa kipindi cha tatu, waliongoza juhudi za kufufua Jumuiya ya Kaunti za Pwani, iliyofifia baada ya kuanzishwa mnamo 2015.

Kwenye mkutano huo eneo la Mwakishimba, Taita Taveta, wawili hao waliungana na mwenyeji wao Granton Samboja na Gavana Dhadho Godhana (Tana River), kujadili mikakati ya kuendeleza muungano huo ili kuleta maendeleo katika eneo hilo.

Huku vigogo wa kisiasa wa kitaifa waking’ang’ania kura za eneo la Pwani, viongozi hao waliapa kutokubali kutumiwa kisiasa katika uchaguzi ujao.

Alhamisi, Bw Joho alitangaza azma ya kuwania urais kupitia chama cha ODM. Akihutubia wanahabari, gavana Samboja alisema kuwa walikubaliana kuwa eneo hilo halitaendelea kudhalilishwa kisiasa kama awali.

“Tumekubaliana kuwa tutakuwa katika meza ambayo maswala ya nchi yanajadiliwa,” alisema.

“Tutafanya kazi pamoja na tutaongoza ili kuafikia malengo yetu,” akasema Bw Samboja. Jumuiya ya Kaunti za Pwani iliyoanzishwa 2015 ilinuia kuleta pamoja kaunti zote za Pwani ili kuwezesha eneo hilo kufanya maendeleo, kukuza uchumi na kuboresha maisha ya wenyeji.

Hata hivyo, muungano huo ulififia kutokana na tofauti za kisiasa za viongozi wa eneo hilo.

Mkurugenzi wa Jumuiya hiyo ni Bw Emmanuel Nzai.

Gavana Samboja alichaguliwa kama mwenyekiti wa muungano huo ili kufufua mikakati iliyokuwa imekwama kutokana na changamoto za hapo awali.

You can share this post!

MCAs wakabiliana wakijadili mswada wa BBI

Muthama, Kalonzo wakashifiwa kwa kujibizana haflani