• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 8:50 AM
CHOCHEO: Utachombeza au kuyatema Valentino hii?

CHOCHEO: Utachombeza au kuyatema Valentino hii?

Na BENSON MATHEKA

KESHO ni siku ya wapendanao na Jenny anasema hatakuwa na raha kwa sababu mpenzi wake Ted hakumtimizia aliyotaka mwaka jana.

“Nilitarajia anipose lakini hakufanya hivyo. Nimevunjika moyo kwa sababu hata mwaka huu haonyeshi nia ya kunioa,” asema Jenny.

Mwanadada huyu asema Ted hampi sababu za kuchelewa kumuoa licha ya uhusiano wao kudumu kwa miaka mitao sasa.

“Marafiki zangu wamekuwa wakiolewa baada ya kuchumbiwa kwa muda wa chini ya miaka mitatu, nimevumilia vya kutosha na asiponipa mwelekeo kesho, nitamuacha,” asema Jenny.

Matarajio yake si tofauti na ya Scola, 27, ambaye amekuwa akisubiri mpenzi wake wa miaka sita amvishe pete ya posa bila mafanikio.

“Sitaki kuharibu muda zaidi. Ikiwa hatanipa mipango ya kunioa mwaka huu, nitabanduka,” asema.

Jenny na Scola hawako peke yao. Nic, mwanamume mwenye umri wa miaka 30 anasema mpenzi wake wa miaka minne, amekuwa akijivuta anapotaka waoane.

“Kila wakati nikimtaka tuanze mipango ya ndoa, huwa anasema tusubiri kwanza. Niko na kazi nzuri na ningetaka kutumia valentino mwaka huu kupata uamuzi wa mwisho kutoka kwake. Hii chelewa chelewa itavuruga mipango yangu ya maisha,” asema Nic.

Hawa ni baadhi ya watu ambao wanatarajia makubwa kutoka kwa wachumba wao siku ya wapendanao mwaka huu.

Kupima mapenzi

Wanasaikolojia wanasema kwamba watu huwa wanatumia siku hii kupima mapenzi ya wenzao kwao.

“Nazungumzia wale ambao wanaendelea kuchumbiana. Wengi wao, hasa vipusa, huitumia kupima kiwango cha mapenzi cha wenzi wao. Kuna wale wanaopima mapenzi kwa kutegemea zawadi wanazonunuliwa, wengine wanaamini wanapendwa kwa kupelekwa deti kali maeneo ya kifahari na wengine wanapima mapenzi ya wenzao wakiwavisha pete ya posa siku ya leo,” asema mwanasaikolojia Damaris Kawira wa shirika la Christ Apple jijini Nairobi.

Anasema wanaotarajia wachumba wao wawaeleze mipango ya kuoana siku ya valentine wanaweza kuvunjika moyo wakikosa kutimiziwa matarajio yao hasa ikiwa uhusiano wao umedumu kwa miaka mingi.

“Japo hii ni siku ya kusherehekea mapenzi, ushauri wangu ni kwamba usishinikize mtu akupe ahadi ya ndoa. Matarajio yanaweza kuwa mengi lakini katu usijaribu kumlazimisha akuvishe pete ya posa iwe siku ya valentino au siku nyingine ile,” asema.

Wanasaikolojia wanasema kuvunja uhusiano siku ya wapendanao kunaweza kuwa na athari zake kwa anayeachwa.

“Sio kwamba haiwezekani lakini sio vyema kukutana na mtu siku inayotazamiwa kuwa ya kusherehekea mapenzi na kisha umpe habari za kumtema. Heri ufanye hivyo kabla ya siku hiyo au ukose kukutana naye kabisa kisha baadaye umfahamishe sababu ya kuvunja deti,” asema Leticia Kananu, mshauri wa masuala ya mapenzi katika shirika la Maisha Mema jijini Nairobi.

Kulingana na Kananu kuacha mchumba siku ya wapendanao ni kumuachia donda la moyo. “Hii inafaa kuwa siku ya raha, ya kutathmini uhusiano wenu, kuufanya upya na kuutia nguvu,” asema.

Ingawa inafaa kuwa siku ya kusherehekea penzi la dhati, watu wengi wameibadilisha kuwa siku ya kulishana uroda na watu wanaowamezea mate.

“Ikiwa wewe ni mwanamke, usitumie siku hii kumlisha tunda mwanamume anayekumezea mate ukidhani atakupenda. Hayo ni matarajio hewa yanayofanya wengi kujuta,” asema.

Haya ndiyo makosa aliyofanya Dina Avendi, mwanadada mwenye umri wa miaka 26.

“Nilidhani kwa vile James alikuwa amenirushia chambo kwa siku nyingi baada ya kuachana na mpenzi wake wa awali, kumburudisha siku ya wapendanao kungemfanya awe wangu. Baada ya usiku huo hakunichangamkia tena na nikabaini alichotaka ni asali tu,” asema Avendi.

You can share this post!

Uhuru aomba talaka

FUNGUKA: ‘Kijogoo mtaani, sichoki kuwika’