• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Kiunjuri abadilisha wimbo, sasa asakata Reggae ya BBI

Kiunjuri abadilisha wimbo, sasa asakata Reggae ya BBI

Na JAMES MURIMI

ALIYEKUWA waziri wa Kilimo Mwangi Kiunjuri, amebadili msimamo wake kuhusu Mpango wa Maridhiano (BBI) na kuwataka Wakenya kupitisha mswada huo kupitia kura ya maamuzi.

Kiongozi huyo wa chama cha Service Party (TSP) na mwandani wa Naibu wa Rais William Ruto, amekuwa akipinga vikali mswada wa BBI unaoungwa mkono na Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga.

“Nimechunguza mswada wa BBI na nimebaini kuwa asilimia 80 ya mambo yaliyomo kwenye mswada huo ni sawa kabisa. Mimi na Naibu wa Rais tumeamua kutopinga BBI.

“Mtu yeyote anayejaribu kutusukuma tupinge BBI atapata aibu. Hatutapinga ng’o,” akasema Bw Kiunjuri katika mahojiano na runinga moja ya humu nchini.

Msimamo wa Bw Kiunjuri uliambatana pia na kauli ya Naibu Rais William Ruto, ambaye alisema kuwa hatajiingiza kwenye mtego ambapo atachukua hatua itakayoleta mgawanyiko nchini. Dkt Ruto alisema hayo jana akiwa katika Kaunti ya Narok.

Bw Kiunjuri anaamini atakayemrithi Rais Kenyatta mwaka ujao, atatekeleza mabadiliko yaliyomo kwenye mswada wa BBI.

“Mabadiliko yaliyomo kwenye mswada huo yatafaidi Wakenya wote na wala si viongozi wachache. Kiongozi wa nchi atakayechukua hatamu za uongozi baada ya Rais Kenyatta kustaafu, atatekeleza mapendekezo yaliyomo katika Mswada wa BBI,” akasema.

“Hakuna serikali mbili. Rais Kenyatta ametekeleza majukumu yake vyema. Tunahimiza mrithi wake kuhakikisha kuwa asilimia 35 ya mapato ya nchi inapelekwa katika kaunti kama ilivyopendekezwa katika Mswada wa BBI,” akaongezea.

Kabla ya kuvuliwa wadhifa wa uwaziri, Bw Kiunjuri mnamo Oktoba 2019, alikutana na kundi la wabunge 42 kutoka eneo la Mlima Kenya katika majengo ya Bunge ambapo waliafikiana kuwa wangepinga ripoti ya BBI.

Baada ya kikao, viongozi hao waliapa kupinga pendekezo la kutaka rais au waziri mkuu kuchaguliwa na wabunge.

Waziri huyo wa zamani alidokeza mwaka jana kuwa atakuwa mwaniaji mwenza wa Dkt Ruto katika Uchaguzi Mkuu ujao.

Jana, alisema kuwa atashukuru Mungu iwapo atateuliwa na Dkt Ruto kuwa mwaniaji mwenza wake.

Mbunge huyo wa zamani wa Laikipia Mashariki, alishikilia kuwa eneo la Mlima Kenya ni sharti litoe mwaniaji mwenza ambaye atapigania masilahi yao katika serikali ijayo.

“Nimekuwa nikisikia uvumi kwamba ninalenga kuwa mwaniaji mwenza wa Dkt Ruto, lakini mimi sijawahi kutamka hilo. Lakini ikiwa hivyo, basi yatakuwa mapenzi ya Mungu ambayo hayawezi kuzuilika,” akasema Bw Kiunjuri.

Aliongeza, “Siasa za 2022 zimeshika kasi lakini sisi watu wa jamii ya Wakikuyu tumenyamaza tu. Tunafaa kuanza mikakati ya kutafuta mtu atakayetuwakilisha serikalini.”

You can share this post!

Kibo Queens invyokuza vipaji kuwa mastaa

Mwaniaji wa udiwani wa UDA akamatwa kwa kuhonga wapigakura