• Nairobi
  • Last Updated May 7th, 2024 9:48 PM
Kibo Queens invyokuza vipaji kuwa mastaa

Kibo Queens invyokuza vipaji kuwa mastaa

NA ABDULRAHMAN SHERIFF

SOKA ya wanawake imenawiri katika jimbo la Pwani, kila kaunti ikijitahidi kutoa wanasoka wenye vipaji wanaopigania fursa ya kuchezea klabu kubwa za Ligi Kuu ya Kenya.

Ni lengo la kila klabu kuhakikisha inafikia kucheza katika ligi kuu ya nchi iliyoko. Mbali na timu kadhaa kuwa na matatizo ya kukosa udhamini, lakini hujitahidi na kubambanya kuhakikisha inafika mbali katika ushiriki wake katika ligi zinazotambulika.

Mojawapo ya klabu za soka ya wanawake ambayo inajitahidi kuhakikisha inashiriki kwenye Ligi ya Kaunti ya Taita Taveta ya FKF ya msimu huu wa 2021-2022 ni Kibo Queens FC, yenye mashabiki wenye kupenda kuwashuhudia wasichana wao wakiendeleza vipaji vya uchezaji wao.

Mashabiki hao ambao ni wakazi wa Kijiji cha Kivukoni kilichoko eneo la wadi ya Chala katika Kaunti Ndogo ya Taveta wamekuwa wakiwaunga mkono wasichana wao ili waweze kushiriki katika ligi hiyo ambayo inahitaji udhamini wa kutosha.

Kocha Mkuu wa Kibo Queens FC, Japhet Atulo anasema wana nia kubwa ya kufika mbali kisoka lakini wanahitaji udhamini sababu ligi wanayoazimia kushiriki inahitaji timu kusafiri na hivyo wanahitaji pesa za kutosha kugharamia safari na mahitaji mengine.

“Nina kikosi imara cha wasichana, wengi wao wanafunzi wa shule ambao wana uwezo mkubwa wa kusakata soka la hali ya juu lakini kunahitajika udhamini ambao utaifanya timu yetu hiyo iweze kupiga hatua ya kujiendeleza na kuweza kupanda ngazi hadi ya Ligi ya jimbo la Pwani.

“Tuliwahi kushiriki kwenye mashindano mengi makubwa kwa nia ya kuwafanya wanasoka wetu watambulike lakini hatujawahi kushinda mataji ambayo tumepania mara hii kuyanyakuwa. Tunataka tuwike huku kwetu ili tukuze vipaji vitakavyoinua jina la sehemu yetu hii,” akasema Atulo.

NYOTA MPYA

Kila wakati, sehemu hiyo imekuwa ikitoa mastaa wapya na kwa wakati huu, hakukukosekana kuwako kwa staa ambaye anatarajia kuwika huku mwenyewe akiwa na nia ya kufika hadi kucheza soka la kulipwa huko barani Ulaya.

Staa huyo ni Leila Joseph aliye nahodha wa klabu hiyo ya Kibo Queens ambaye nia yake kubwa ni kuhakikisha yeye na baadhi ya wenzake wanafika kucheza soka la kutambulika, kwanza kuchezea timu ya taifa ya soka ya wanawake ya Harambee Starlets na baadaye kwenda ng’ambo.

“Nia yangu na wenzangu ni kuhakikisha tumefanikiwa kushiriki Ligi Kuu ya Soka ya Wanawake hapa nchini ama wengi wetu tufikie viwango vya kujiunga na klabu za ligi kuu kwani ndipo tutapata fursa ya kuonekana na kuchaguliwa kwa timu ya Harambee Starlets,” amesema Leila.

Msichana huyo amewahi kuichezea timu ya Taveta Estate iliyowahi kushiriki kwenye mashindano ya Governor’s Cup ambapo fainali zake zilifanyika uwanja wa Dawson mwanyumba na ambayo iliweza kufika fainali na kuwa mshindi wa pili.

KIKOSI IMARA

Kocha Atulo anasema ana kikosi imara chenye kuweza kukabiliana na wapinzani wao wowote lakini akatoa ombi kwa wadhamini kujitokeza kuwasaidia ili wasichana wake wasikae mitaani bila ya kuwa na la kufanya na wakajitosa kwenye maovu yatakayowaharibia Maisha yao.

Wanasoka wa timu hiyo pamoja na nyingine ya U-17 ni Leila Joseph (Nahodha), Rehema Ramadhani, Alice Kyalo, Winnie Njoki, Mariam Wakio, Roda Akoth, Agnes Doreen, Anna Peter na Damaris Wayuwa.

Wanasoka wengine ni Doreen Jibran, , Dorothy Kileleji, Gloria John, Linantoz Mwambi, Faith Mbogholi, Mariam Suleiman, Wanjala Mwanyalu, Stella Kariuki, Abigael Mnyeri na Cristine Ndungu.

Atulo amepania kukiongoza kikoais chake hicho kwenye ufanisi huku akiwa na matuamini makubwa ya kuhakikisha miongoni mwa wanasoka hao wanafikia malengo yao ya kucheza soka la kulipwa huko barani Ulaya.

  • Tags

You can share this post!

Kingi amzima Raila

Kiunjuri abadilisha wimbo, sasa asakata Reggae ya BBI