• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 3:25 PM
Ana matumaini tele kushiriki katika raga ya hadhi akifuata nyayo za Collins Injera

Ana matumaini tele kushiriki katika raga ya hadhi akifuata nyayo za Collins Injera

Na PATRICK KILAVUKA

MCHEZO wa raga hauhitaji tu usuli na nguvu bali unahitaji ujuzi na mazoezi si haba kuhimili makali yake.

Hii ni kauli ya mwanaraga Campbell Okello, 17, mwanafunzi wa Kidato cha Pili katika Shule ya Upili ya Sigome, Kaunti ya Siaya.

Alianza kuwa na hamu ya kuujua mchezo huu tangu akiwa katika Darasa la Sita katika Shule ya Msingi ya Buruburu 1, Kaunti ya Nairobi.

Alijenga imani mchezoni kutokana na vile alikuwa anaona ukichezwa hadi akanuia kuanza kutafuta mengi kuhusu kwenye mtandao wa youtube na kuhudhuria ukichezwa uwanjani.

Mchezaji wa hadhi ya kitaifa na kimataifa Collins Injera anampa kiu na hamasa ya kutia bidii mchezoni.

Anasema alipokuwa anamuona mchezaji huyo akichapa shughuli ugani, alikuwa anasisimuka kiasi cha kuweza kuongezea matumaini kuwa hai siku moja atashiriki katika ulingo wa fani hii mithili yake au kufuata nyayo zake unyounyo.

“Mimi hujifua zaidi ninapokuwa uwanjani kwani kupitia mazoezi makali, nimepata kushiriki katika mashindano ya shule za upili hadi kiwango cha kaunti kabla msambao wa ndwele ya corona,” anasema mchezaji huyo ambaye hucheza kama mwanaraga kiungo.

Isitoshe, alijiunga katika timu ya shule akiwa kidato cha kwanza, muhula wa tatu.

Mwanaraga Okello anasisitiza kwamba, pindi tu alipojiunga na shule ya upili, alijaribu kutathmini mchezo upi angejiunga kuucheza! Lakini dau lake halikuzama kwani, alimpata kocha Joel Ambani ambaye huinoa timu ya shule na akamshawishi kujiunga.

Mwanaraga Campbell Okello (kushoto) wa timu ya raga ya Umoja Innercore akiwa na mchezaji Andrew Njagi. Picha/ Patrick Kilavuka

Kwa vile alikuwa na ari tangu awali na mapenzi makubwa katika mchezo huu akiwa shule ya msingi, aliamua kulivalia njuga azimio lake na kujiunga na timu ya shule chini ya kocha huyo ambaye kwa sasa amemuamini nafasi katika kikosi cha kwanza na anafanya mambo kweli pasi na shauku.

Chini ya mkufunzi Ambani ambaye anamlea kipaji, anasema anaona atafikia upeo wa kuchezea timu za haiba nchini mfano KCB ambayo moyo wake unamdekadeka kuichezea kabla kuazimia kuyoyomea nchi za Afrika Kusini, Ufiji, Austraila au Unigereza ambako mchezo huu umekita mizizi.

Yeye hufanya mazoezi yake katika awamu tatu. Huanza saa 5.00 -5.30 am kwa kukimbia, 6.00 – 7.00 am mazoezi ya kupasha misuli na viungo na 8.00 – 9.00 am huchukua fursa ya kutizama mazoezi ya kujiweka mufti kwenye youtube na kuona jinsi anavyoweza kuyasawzisha kwenye yake mazoezi.

Kwingineko, huzoa maarifa ya kujinyanyua zaidi kutoka kwa kocha Ambani ambaye pia huchezea timu ya Rhino, Kaunti ya Kakamega.

Hata hivyo, kando na kupiga zoezi shuleni na kucheza, wakati wa likizo, hupata mwanya wa kuyaendeleza makali yake katika timu ya raga ya Umoja Innercore, mtaani Tena jijini Nairobi.

Yeye huhimizika sana kutia wengine motisha katika kukuza mchezo huu na anamnoa mchezaji Stower Otieno.

Anasema humtia mori ya kucheza kwa bidii ya mchwa kudhihirisha kwamba ana uwezo katika mchezo ili, azoe ujuzi, awe ari na kujiepusha na mawazo potovu kwamba, mchezo huu ni mgumu na hatari unapouchezea.

“Mimi humzindua kuzingatia mazoezi na kuendeleza kiu ya kuujua kwani unapopata majereha ni njia moja ya kujiimarisha na changamoto za mchezo,” asema mchezaji Okello.

Amewahi kufunga trai 30 na kwa kila mchezo, anasema yeye hujitahidi ukucha kwa jino kufunga zaidi ya trai moja.

Ana ndoto ya kukaa mkaao na wachezaji miamba kama mwanaraga Injera siku moja kupata mawili matatu ya kimaarifa.

Bonge la ushauri kwa wengineo wanaotaka kuvaa jezi ya raga ni kwamba, mchezo wa raga si mgumu mithili ya mwamba ila, ujuzi, ari na bidii ya mchwa mazoezi ndivyo vigezo muhimu vya kukuwezesha kufaulu!

You can share this post!

AKILIMALI: Mlinzi anayevuna pato kwa kukuza sukumawiki za...

Liverpool waafikiana na RB Leipzig kumsajili beki Konate...