Na GEOFFREY ANENE
MIAMBA wa mpira wa vikapu nchini Kenya, KPA walianza mashindano ya mwaliko ya Mzuri Zaka kwa kishindo nchini Malawi mnamo Jumamosi.
Wanaume wa KPA walikuwa wa kwanza kujibwaga ukumbini Blantyre. Walipepeta Crazy Warriors kwa alama 87-31 katika mechi ya ufunguzi kabla ya kuongeza Poly & Bricks katika orodha ya majeruhi kwa kuwalima 84-40.
Nao kinadada wa KPA walinyamazisha Kukoma Eagles 106-25 kabla ya kuzidia ujanja Mikoko Mystics 82-22. Medina Okot alikuwa fundi wa KPA kubomoa Kukoma alipochangia alama 35.
Timu ya KPA ya wanawake, ambayo inatiwa makali na Anthony Ojukwu, inatarajiwa kurejea uwanjani kumenyana na Cobbe baadaye leo. Cobbe ilipoteza mechi dhidi ya Mystics kwa kuchelewa kufika uwanjani. KPA wanaume watalimana na Magang’a. Mashindano hayo ni ya juma moja.