• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Utalii wapigwa jeki Lufthansa ikizindua safari

Utalii wapigwa jeki Lufthansa ikizindua safari

Na SIAGO CECE

SEKTA ya utalii nchini imepigwa jeki baada ya Kenya kupokea ndege ya watalii kutoka Frankfurt, Ujerumani katika uwanja wa ndege wa Moi mjini Mombasa.

Ndege hiyo ni ya kwanza aina ya Eurowings kutoka kampuni ya Lufthansa, iliyotoka Ulaya na ilikuwa imebeba watalii 150.

Akizungumza mjini Mombasa baada ya kukaribisha ndege hiyo Jumapili alfajiri, Katibu Mkuu wa Wizara ya Utalii, Bi Safina Kwekwe alisema safari hiyo imeleta matumaini kwa sekta ya utalii iliyokuwa imedidimia tangu janga la virusi vya corona lilipoanza kutikisa dunia.

Ndege hiyo itakuwa ikitua Mombasa mara mbili kwa wiki, Jumapili na Alhamisi.

“Katika serikali, tunajitahidi kuhakikisha kuwa tuko tayari kukaribisha watalii wengi nchini Kenya,” Bi Kwekwe alisema.

Balozi wa Ujerumani humu nchini, Bi Annette Gunther ambaye alikuwa Mombasa kuilaki ndege hiyo alisema safari hiyo ya ndege inaashiria pia uhusiano mwema ulioko kati ya nchi ya Kenya na Ujerumani.

Watalii Wajerumani wamekuwa wakitembelea maeneo ya Kenya hasa Pwani kwa miaka mingi na baadhi yao wamefanya miji kama vile Malindi na Mtwapa kuwa makao yao.

“Kampuni nyingi ambazo zinakuja kufanya biashara Kenya huwa haziondoki, na tunajua pia ndege hii haitakuwa ya mara moja tu bali itaendelea kwa miaka ijayo,” Bi Gunther alieleza.

Itakapofika mwaka ujao, ndege hiyo itaanza kutua Mombasa mara nne kwa wiki.

Wadau katika sekta ya utalii nchini Kenya pia wamefurahia kuja kwa ndege hiyo wakisema kuwa wanatarajia ndege zaidi za kukodisha kutua Mombasa.

“Tumeona katika siku za hivi majuzi idadi ya watalii kutoka nchi za nje inaongezeka. Hii ina maana kuwa sekta hii yetu iliyokuwa imeathirika na janga la corona itaimarika,” alisema Bw Wasike Wasike, ambaye ni naibu mwenyekiti wa Chama cha Wahudumu wa Hoteli (KAHC).

Alisema hoteli nyingi zimejiratayarisha ipasavyo kuhakikisha kuwa afya ya wageni wao ni salama kwa kuzuia maambukizi ya virusi vya corona.

Tangu mwaka 2020, maelfu ya wafanyikazi wa hoteli na mashirika mengine ya utaliii walipoteza kazi baada virusi vya Corona kuongeza na kusababisha nchi nyingi kukomesha usafiri wa nje.

Eneo la Pwani linategemea sana watalii wa kigeni, mara nyingi wakazi hufanya biashara na watalii hao na mwishowe kujiendeleza kimaisha.

You can share this post!

Uchaguzi: Mrengo wa Ruto watishia kushtaki Kenya UN

Mulembe wapigania minofu ya Uhuru