• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 10:50 AM
Mtihani manaibu 3 wakiendea ugavana

Mtihani manaibu 3 wakiendea ugavana

MAUREEN ONGALA na VALENTINE OBARA

MANAIBU gavana wa kaunti tatu za Pwani wanatarajiwa kukabiliana na mibabe wa kisiasa mwaka ujao katika uchaguzi wa ugavana.

Gavana Hassan Joho wa Mombasa, Amason Kingi (Kilifi) na Salim Mvurya (Kwale) wanatumikia kipindi cha pili cha uongozi ambacho ni cha mwisho kikatiba.

Manaibu wao ambao ni Dkt William Kingi (Mombasa), Bw Gideon Saburi (Kilifi) na Bi Fatuma Achani (Kwale) tayari wametangaza maazimio ya kurithi viti hivyo.

Kufikia sasa, ni Bw Mvurya pekee ndiye ambaye amejitokeza wazi kuunga mkono azimio la Bi Achani kati ya magavana hao watatu.

Mabw Kingi na Saburi wana imani kura ya mchujo itafanywa kwa njia huru na ya haki jinsi walivyoahidiwa na kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga.

Katika Kaunti ya Kilifi, Bw Saburi anatarajiwa kumenyana na Waziri Msaidizi wa Ugatuzi, Bw Gideon Mung’aro kwenye mchujo wa ODM.

Bw Mung’aro aliwania ugavana 2017 kupitia chama cha Jubilee, akapata kura 56,547 dhidi ya kura 218,686 za Gavana Kingi.

Mbali na Bw Mung’aro, Mbunge wa Malindi, Aisha Jumwa, balozi wa Kenya nchini Tanzania, Bw Dan Kazungu ni miongoni mwa wanasiasa wengine.

Hata hivyo, alisema hatishiwi na wanasiasa wanaomezea mate kiti hicho.

“Kufikia sasa ni mimi pekee ambaye nimetangaza nia ya kuwania ugavana Kilifi kupitia ODM. Tayari niko ndani ya serikali na nitaendeleza kazi aliyoanzisha bosi wangu,” akasema.

Katika Kaunti ya Mombasa, Dkt Kingi anatarajiwa kupigania tikiti ya ODM dhidi ya Mbunge wa Mvita, Abdulswamad Nassir na mfanyabiashara Suleiman Shahbal.

Bw Shahbal aliwania ugavana 2013 na 2017 kupitia Chama cha Wiper na Jubilee mtawalia lakini akashindwa na Bw Joho.

Mbali na hao, kiti hicho kimevutia pia aliyekuwa seneta wa Mombasa, Hassan Omar na Mbunge wa Kisauni Ali Mbogo, ambao ni wafuasi wa Chama cha UDA kinachohusishwa na Naibu Rais William Ruto.

“Sote tutakutana debeni na kila mmoja wetu atapigania nafasi yake na nitaibuka mshindi. Nimekuwa naibu gavana kwa miaka minne sasa na tumefanikisha mambo mengi kwa jamii,” akasema Dkt Kingi.

Kufikia sasa, wabunge wengi wa ODM Mombasa wametangaza kumuunga mkono Bw Nassir, huku madiwani na washirika wa karibu wa Bw Joho wakiegemea upande wa Bw Shahbal.

Katika Kaunti ya Kwale, Bi Achani ambaye ni mwanachama wa Jubilee hajatangaza ikiwa atatumia chama hicho kuwania ugavana mwaka ujao au la.

You can share this post!

Wanawake sasa walilia usalama katika kampeni

Kitita cha Sh.6Milioni kilipatikana katika afisi za majaji...