• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Covid: Wadau wa utalii walalama kubaguliwa

Covid: Wadau wa utalii walalama kubaguliwa

Na WACHIRA MWANGI

WADAU katika sekta ya utalii wamelalamika kuwa sekta ya utalii inabaguliwa serikali inapoendelea kujaribu kurejesha hali ya kawaida ya kimaisha kipindi cha janga la corona.

Hii ni baada ya serikali kutangaza itaruhusu magari ya uchukuzi wa umma kubeba abiria kwa viti vyote kuanzia leo.

Wasimamizi wa hoteli maeneo ya Pwani wameitaka serikali ilegeze kamba kuhusu kanuni za kupambana na virusi vya corona ambazo zinaathiri sekta ya utalii.

Afisa mkuu katika Chama cha Wahudumu wa Hoteli, Dkt Sam Ikwaye alisema sekta hiyo imeathirika sana na sera za serikali zilizonuia kuepusha maambukizi ya virusi vya corona ikilinganishwa na sekta nyingine za kibiashara na kijamii.

“Tunataka mkutano na maafisa wa wizara za afya na utalii ili tupate mwelekeo kuhusu sekta hii. Mwaka mzima wa 2020 ulikuwa wa hasara, hivi sasa 2021 inakaribia kukamilika kwa hasara. Ifikapo 2022 itakuwa ni mwaka wa kisiasa, tutafufua vipi biashara zetu baada ya 2022?” akauliza.

Sekta ya utalii ni miongoni mwa zile zilizoshuhudia maelfu ya watu wakipoteza ajira hasa katika maeneo ya Pwani kwa sababu ya upungufu wa watalii.

Hali hiyo ilisababishwa na sera ambazo zilifanya iwe vigumu kwa watu kusafiri kitaifa na kimataifa, sera kuhusu idadi ndogo ya watu wanaotakikana kukubaliwa kukutana kwa wakati mmoja na wakati mwingine marufuku ya mikutano ya ana kwa ana, kufungwa kwa maeneo ya burudani yaliyokuwa vivutio vya utalii, na sheria kali za kudhibiti mikahawa na baa.

Dkt Ikwaye alilalamika kuwa wafanyabiashara katika sekta hiyo sasa wamegeuka ombaomba wanapojaribu kuendeleza maisha yao.

Alisema wamiliki wengi wa hoteli waliwekeza pesa nyingi ili kuhakikishia wageni usalama wao dhidi ya Covid-19 lakini bado serikali haitaki waendeleze biashara kama ilivyokuwa kawaida ilhali sekta nyingine zinaruhusiwa.

Meneja Mkuu wa Hoteli za kenya Safari, Bw Joseph Ndunda, alisema sekta hiyo inabaguliwa kwani nyingine ambazo hata hazifuati kanuni ipasavyo zinaruhusiwa kuendeleza biashara kama kawaida.

Jumanne iliyopita, Waziri wa Utalii, Bw Najib Balala alitangaza mikakati mipya inayolenga kufufua utalii wakati huu wa janga la corona, lakini wawekezaji katika sekta hiyo wanalalamika kuwa serikali haijamakinika katika suala hilo.

Mojawapo ya mipango aliyotangaza ni kuwapa kipaumbele wahudumu wa hoteli kupokea chanjo ya kuwalinda dhidi ya Covid-19.

You can share this post!

Raila amsuta Ruto kulialia ndani ya serikali

Kega akemea Msajili kuhusu waasi JP