• Nairobi
  • Last Updated May 7th, 2024 9:48 PM
Raila amsuta Ruto kulialia ndani ya serikali

Raila amsuta Ruto kulialia ndani ya serikali

Na WAANDISHI WETU

KIONGOZI wa Chama cha ODM, Bw Raila Odinga, amemsuta Naibu Rais William Ruto kwa kulalamika jinsi rafiki yake, Bw Harun Aydin, alikamatwa na maafisa wa kupambana na ugaidi.

Bw Odinga alisema ni kinaya kwamba wanaolalamika wako ndani ya serikali na wanajua yanayojiri, ilhali wanataka kulaumu wengine.

Bw Aydin alikuwa aandamane na Naibu Rais kuelekea Uganda wiki iliyopita; lakini Dkt Ruto alizuiwa kusafiri, ikidaiwa kuwa amri ya kutaka asiondoke nchini ilitolewa na mamlaka za juu serikalini.

Raia huyo wa Uturuki alikamatwa na polisi Jumamosi katika uwanja wa ndege wa Wilson jijini Nairobi, akitokea Kampala, Uganda.

“Serikali inashughulikia mambo ya uhalifu na kadhalika. Wale ambao wako serikalini lakini wanapiga kelele ndio wanajua kinachoendelea na sababu zake. Mimi siwezi kujua kama sijaelezwa maana siko serikalini,” alisema Bw Odinga.

Alikuwa ameandamana na Mbunge wa Mvita Abdulswamad Nassir na Naibu Gavana wa Mombasa, Dkt William Kingi, kwa ibada katika kanisa la ACK Mombasa.

Dkt Ruto na wanasiasa wanaoegemea upande wake jana waliendelea kulalamika kuhusu kisa hicho, wakidai ni sehemu ya mbinu za kumhangaisha katika safari yake ya kuwania urais mwaka 2022.

Akiongea baada ya kuhudhuria ibada katika kanisa Katoliki la St Joseph mjini Naivasha, Kaunti ya Nakuru, Dkt Ruto alisema wanaompiga vita kisiasa watumie nguvu zao kuunganisha Wakenya na kuuza manifesto zao.

“Mipango yetu ya maendeleo haikupiga hatua kubwa kwa sababu ya migogoro ya kisiasa. Sasa wanataka kutisha Wakenya kwamba, ukiwa rafiki wa Ruto utapelekwa mahakamani. Kama wewe ni mwekezaji unayejuana na Ruto utapelekwa mahakamani,” akaeleza.

Mbunge wa Kikuyu, Bw Kimani Ichung’wa, alishutumu baadhi ya maafisa katika Ofisi ya Rais akidai wanahusika kumdhalilisha Dkt Ruto.

Akisema ni ofisi hiyo ambayo hushughulikia suala la kuwapa raia wa kigeni idhini ya kuingia nchini, alishangaa vipi Mturuki huyo alikubaliwa kuingia Kenya na kuondoka mara kadhaa hapo awali.

Bw Ichung’wa alionya kwamba kisa cha hivi majuzi kitafukuza wawekezaji nchini, huku akimsihi Naibu Rais kusimama kidete na kutotishwa na mipango ya wapinzani wake.

“Walianza na viongozi wanaoegemea upande wa Naibu Rais. Lakini sasa wamehamia wawekezaji na wafanyabiashara mpaka wawekezaji sasa wanatoroka nchi,” alihoji.

Duru zilisema Bw Aydin anatarajiwa kufikishwa mahakamani leo; na polisi wataomba kumzuilia kwa muda zaidi ili wakamilishe uchunguzi kuhusu madai kwamba anahusika katika kufadhili ugaidi.

Mwaka huu 2021, inasemekana Mturuki huyo amesafiri Kenya mara sita kutoka Istanbul (Uturuki), Cairo (Misri) na Addis Ababa (Ethiopia).

Wakili wake, Bw Ahmednassir Abdullahi, Jumapili alisema bado hajakubaliwa kumwona.

“Kwa siku ya pili nimekatazwa kumwona Harun Aydin. Sababu bado ni ile ile…“amri kutoka juu”. Kwa bahati nzuri, hawana budi ila kumfikisha mahakamani kesho (leo Jumatatu) kama inavyotakikana kikatiba,” akasema kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter.

Afisa katika ubalozi wa Uturuki jijini Nairobi alisisitiza kuwa, Bw Aydin hana rekodi yoyote ya uhalifu nchini kwao na ni mfanyabiashara. Hata hivyo, hajasema hufanya biashara gani.

Ripoti za Winnie Atieno, Mary Wambui na Macharia Mwangi

You can share this post!

Musyoka akoleza urafiki wa kisiasa na Lenku

Covid: Wadau wa utalii walalama kubaguliwa