• Nairobi
  • Last Updated April 25th, 2024 8:55 PM
Mfumo wa kuinua uchumi bottom-up umetajwa kwenye Biblia – Ruto

Mfumo wa kuinua uchumi bottom-up umetajwa kwenye Biblia – Ruto

Na SAMMY WAWERU

NAIBU wa Rais William Ruto ameendelea kutetea mfumo wa bottom-up kuboresha uchumi, anaotumia kama mojawapo ya sera kutafuta kura kumrithi Rais Uhuru Kenyatta 2022.

Dkt Ruto amesema mfumo wa kuinua uchumi kutoka chini kuenda juu, anaohoji unalenga maskini, mwananchi wa kawaida na vijana umetajwa kwenye Biblia.

“Wakati mnaskia tunasema kuhusu mfumo wa kuboresha uchumi wa bottom-up, umetajwa kwenye Biblia agano la Zaburi sura ya 113 mlango wa 7 na 8,” Dkt Ruto akasema.

Alisema hayo Jumapili, alipohudhuria ibada ya misa katika Kanisa la Katoliki la Mtakatifu Francis Assisi, Gatina, eneo la Kawangware, Nairobi.

“Mungu aliye juu mbinguni anasema atamwinua fukara kutoka mavumbini, amnyanyue maskini kutoka unyonge wake na kumketisha na wafalme, pamoja na viongozi wa watu wake,” Naibu Rais akanukuu mafungu hayo.

Huku baadhi ya wapinzani wake wakimkosoa na kudai ahadi zake ni hadaa tupu kwa wananchi, Ruto alisema endapo atakuwa rais wa tano wa Jamhuri ya Kenya, mfumo wa bottom-up atautumia kutafutia ajira wasio na kazi, kina mama mboga na kundi la mahastla, kauli anayotumia kuashiria na kujihusisha na “watu wa kiwango cha chini kimaendeleo”, kuboresha maisha yao.

Aidha aliendelea kusuta wapinzani wake, akisema wanatumia Mpango wa Ripoti ya Maridhiano (BBI) ambao hatma yake i mikononi mwa mahakama ya rufaa, kubuni nafasi za uongozi kujinufaisha.

“Nyinyi watu wa Kawangware mtakubali tuwe na mjadala wa kugawana mamlaka?” akahoji wakati akihutubia waumini wa Kanisa la Katoliki la Mtakatifu Francis Assisi, akionekana kuelekeza matamshi yake kwa kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga.

“Utulivu na umoja wa taifa utakuwa wa manufaa endapo mjadala hautaegemea kubuni nafasi za viongozi. Uwe wa kuimarisha maisha ya wananchi…Hapo ndio tutakuwa tunatembea pamoja kama taifa na Wakenya,” akasema.

Naibu Rais ni kati ya viongozi na wanasiasa walioeleza azma yao kuwania urais mwaka 2022.

You can share this post!

Mang’u Youth FC yaendelea kuongoza ligi ya Kanda ya...

AKILIMALI: Avuna hela kutokana na ufugaji sungura na njiwa...