• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 3:31 PM
Polo aliyeungua makalio akificha bangi yenye moto aokoka

Polo aliyeungua makalio akificha bangi yenye moto aokoka

NA MWANGI MUIRURI 

POLO aliyechomeka kupitia bangi iliyokuwa ikiwaka aliyoficha kwenye makalio kukwepa kufumaniwa na polisi, ametangaza uamuzi wa kuokoka na kuapa kumtumikia Mungu.

Kulingana na mdokezi, polo huyo alikuwa katika kundi la vijana wanne ambao walikuwa wakivuta ‘dawa’ hiyo kwa awamu katika mtaa wa Mathare wakati maafisa wa polisi walijitokeza ghafla mwendo wa saa moja jioni.

“Polisi hao walikuwa wamejigawa kwa makundi manne na hakuna vile vijana hao wangetoroka kwa kuwa walikuwa wamezingirwa. Aliyekuwa ameshika bangi hiyo ikiwa imewashwa, alionekana kuchanganyikiwa lakini akili bunifu zikamwingia ghafla,” mdokezi akaarifu

Inasemekana kwamba jombi alikuwa ameshika msokoto huo kwa mkono wa kulia, kisha ukaonekana ukiingia ndani ya long’i yake kwa upande wa nyuma kupitia kiunoni na ulipotokea nje tena, haukuwa umeshika bangi hiyo.

“Polisi walifika katika kundi hilo na kupata vijana wanne wakiwa wamesimama tu na licha ya harufu ya bangi kutanda hewani, hakuna aliyekuwa na ushahidi wa kuivuta,” mdaku wetu akasimulia.

Hata hivyo, mwathiriwa aliangua kilio cha mahangaiko punde tu maafisa hao walipoondoka na alipokaguliwa na wenzake, akapatikana alikuwa amechomeka katikati ya makalio alikokuwa ameficha bangi.

“Kumbe polo alikumbatia bangi akitumia makalio yake na akavumilia makali ya moto ili kuhepa polisi! Licha ya kuwa unyevu wa jasho maeneo alikokuwa ameficha bangi ulikuwa umeizima, alikuwa tayari amechomeka vibaya,” msimulizi akasema.

Kalameni alisikika akitangaza kwamba hiyo ndiyo ilikuwa siku yake ya mwisho kuvuta bangi na kwa uhakika, tangu siku hiyo hajaonekana katika mtaa huo alikochomea makalio akiificha polisi.

Duru zinaarifu, anaonekana akiwa katika urafiki wa waliookoka.

[email protected]

  • Tags

You can share this post!

Dorice Aburi: Nilikuwa ninajizungumzia

Polisi wanasa bangi ya Sh320, 000 Bomet

T L