• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 7:55 AM
Dorice Aburi: Nilikuwa ninajizungumzia

Dorice Aburi: Nilikuwa ninajizungumzia

NA WYCLIFFE NYABERI

WAKENYA kwenye mitandao ya kijamii wamemvamia na kumkashifu vikali Mwakilishi wa Kike Kaunti ya Kisii, Dorice Aburi baada ya kuchapisha video yenye maneno makali kwa mlinzi wake ambaye inadaiwa “alifiwa”.

Desemba 26, 2023, Bi Aburi kupitia ukurasa wake rasmi wa Facebook alichapisha video ya sekunde 82 ambapo anaskika akimkaripia mlinzi wake kwa kutoripoti kazini kwa wiki tatu.

Bi Aburi, maarufu kama Donya Toto, aliipa video hiyo ambayo sasa inasambazwa kwa kasi mitandaoni anwani ‘Useless officer’, lakini amejikuta pabaya akikashifiwa na wafuasi wake na wanamitandao wanaosema kiongozi huyo alikosa “utu”.

Katika mazungumzo ya simu, baina yake na mlinzi huyo, mwanahabari huyo aliyejitosa siasani baada ya kupata umaarufu alipokuwa mtangazaji wa redio moja maarufu inayopeperusha matangazo yake kwa Ekegusii, anamuuliza mlinzi alikokuwa kwa kipindi hicho chote bila kuripoti kazini.

Mlinzi huyo anamjibu kwamba hakuwa amerejea kazi kwa sababu alifiwa na mkewe.

Huku akikiri kwamba alifahamu kuwa mlinzi wake “alimpoteza” mkewe, Bi Aburi alisema mazishi yake yalikuwa yamekamilika wiki mbili zilizopita na kwa hivyo alitarajia afisa huyo anapaswa kurejea kazini mara moja.

Juhudi za mlinzi huyo kusema hakuwa amepata nguvu za kurejea kazini kufuatia msiba uliomkumba, zilipuuzwa na mbunge huyo ambaye alimuuliza jinsi kifo cha mkewe kinahusiana na kazi yake!

“Afisa, unalipwa kwa kile unachozalisha kazini. Hujafika kazini kwa muda wa wiki tatu…Unaniambia unaomboleza mkeo na najua kabisa ulikuwa ukimuomboleza mkeo na ulimzika wiki mbili zilizopita…Kwa hiyo haukuja kazini kwa sababu ulikuwa ukimuomboleza mkeo?” Bi Aburi aliuliza huku akicheka.

“Nyinyi hamko makini…Sijui watu wana matatizo gani…Sijui kwa kweli,” akasema Bi Aburi, kisha akasitisha mawasiliano.

Baadaye, alianza kuimba wimbo wa Kikatoliki “Asubuhi ya Kupendeza” ambao inaonekana alikuwa ameusimamisha usicheze kutoka kwa kipakatalishi chake ili apige simu hiyo.

Kwenye klipu hiyo, Bi Aburi amevalia blauzi nyeusi akiwa na rozari shingoni.

Mkono wake wa kulia unaonekana kufungwa na bendeji nyepesi.

Huku baadhi ya wafuasi wake wakisema mbunge huyo alikuwa akitania, wengine walimshambulia kwa kile walichoeleza kuwa hakumwonea huruma “afisa aliyefiwa”. Hizi ni sehemu tu za jumbe zilizoandikwa na wafuasi wake kwenye safu ya maoni Facebook:

Bwana Simeon Atuti aliandika: “Mheshimiwa Donya Dorice Aburi, unajua jinsi inavyoumiza unapofiwa na mpendwa wako, 2027 ndio mwisho wa safari yako ya kisiasa, hata mbinguni haitazuia anguko lako.”

Naye Denopapa Oshesh alisema: “Ulipoteza maadili. Binadamu ni viumbe wenye hisia. Wewe si huruma. Huzuni ni aina ngumu zaidi ya elimu. Tayari umechagua kiburi kinachohusishwa na msimamo wako. Uvumilivu na kuelewa kuko wapi kama kiongozi?”

Wycliffe H. Omundi alisema: “Kiburi chako ni kitu kingine. Inasikitisha! huzuni!

Jared Nyambega Ekwinini naye aliachangia akisema: “Najua watu wengi hapa hawaelewi kinachoendelea, ngoja nichambue ili uelewe vizuri…”

Kufuatia mlipuko huo, Bi Aburi katika chapisho lingine Facebook alijitetea akisema sarakasi hiyo ilikuwa ya kujizungumzia peke yake, kama vile mhusika katika tamthilia anavyoweza kuzungumza mawazo ya mtu kwa sauti akiwa peke yake au bila kujali msikilizaji yeyote.

“Hakuna hata mmoja wa maafisa wangu aliyefiwa, tusidharau na kukosa ujumbe bali tuelewe muktadha na sio maana halisi ya wazi,” alichapisha Bi Aburi.

 

  • Tags

You can share this post!

Wachuuzi walivyovuna kufuatia msongamano wa magari msimu wa...

Polo aliyeungua makalio akificha bangi yenye moto aokoka

T L