Na RICHARD MUNGUTI
MLINZI aliyechukua picha za video ya mwanamke akiwa msalani akitumia simu ya Smartphone katika kituo kimoja cha mafuta ya petrol jijini Nairobi amesukumwa jela kusubiri kuhukumiwa kwa kuwa msumbufu.
Bawabu huyo Mark Ambeyi Mutongoyi mwenye umri wa miaka 28 alikiri makosa aliposhtakiwa. Akikiri alimpiga mwanamke huyo picha akiwa msalani mshtakiwa alidai alipagawa na pepo aliyemshawishi ampige picha mlalamishi ajifurahishe kwa kumtazama baadaye.
“Ni pepo mbaya aliyeniingia hata nikatamani kumpiga picha mlalamishi,” alisema Ambeyi. Mlalamishi alikiri alisababisha kero kwa kumpiga picha mwanamke huyo katika choo kilichoko kwenye kituo cha mafuta ya petrol cha Rubis mnamo Oktoba 7 mwaka huu.
Mlalamishi alikuwa ameingia katika petrostesheni hiyo kujaza gari lake mafuta. Akiwa msalani mshtakiwa alimpiga picha akimchunguza kupitia mwanya katika mlango wa choo hicho.
Mlalamishi alilalamika kisha mshtakiwa akakamatwa baada ya wasimamizi wa kituo hicho cha mafuta kuchunguza kamera za CCTV. Atahukumiwa Novemba 1, 2021 ripoti ya afisa wa urekebishaji tabia itakapotolewa.
Akijitetea mshtakiwa aliomba asamehewe kwa vile ni baba wa watoto wawili wanaomtegemea pamoja na mkewe.