NA BENSON MATHEKA
BUNGE la Kenya na la Hungary zitaimarisha ushirikiano kwa lengo la kunufaisha nchi hizo mbili.
Hii ni baada ya Spika wa Bunge la Taifa Dkt Moses Wetang’ula, kumwalika mwenzake wa Hungary, Laszlo Kover kuzuru Kenya kwa mazungumzo
Spika huyo wa Bunge la Hungary, yuko nchini kwa ziara rasmi ya wiki moja.
Bw Wetang’ula alishukuru serikali ya Hungary kwa kutoa ufadhili wa masomo kwa Wakenya zaidi ya 200 hatua ambayo alisema itasaidia kubadilisha maisha ya watu kupitia elimu spesheli na ujuzi.
Spika Wetag’ula pia alishukuru serikali ya Hungary kwa kusaidia Kenya katika miradi tofauti akisema nchi hizi mbili zina uhusiano wa miaka mingi.
Kuhusu ushirikiano wa Bunge, Bw Wetang’ula alisema utasaidia nchi zote mbili kubadilishana ufahamu na mawazo katika biashara, Kilimo, Elimu, Tekinolojia, Usalama na Utalii.
“Ushirikiano wa Bunge na Bunge ni muhimu kwa ushirikiano wa nchi na nchi katika mipango tofauti ikiwemo kufanya biashara kwa kuwa Kenya inalenga kupanua ushirikiano wa kibiashara,” akasema Wetang’ula alipompokea Kover katika majengo ya Bunge.
Akisema ni Spika wa kwanza wa Bunge la Hungary kuzuru Kenya kwa ziara rasmi, Laszlo Kover alisema mabunge yana jukumu muhimu kutia nguvu uhusiano wa nchi mbili na akahimiza wabunge kuendelea kuzungumza kuhusu mipango ya maendeleo.