NA SAMMY KIMATU
MWANAMUME mwenye umri wa miaka 49 alifariki Alhamisi baada ya kunywa pombe haramu.
Kisa hicho kilitokea katika eneo la Dallas katika mtaa wa mabanda wa Mukuru-Kayaba ulioko South B, kaunti ndogo ya Starehe.
Akiongea na Taifa Leo, Msimamizi wa zahanati ya Lengo Medical Clinic iliyoko eneo la Lengo mtaani humo, Dkt Kennedy Kipchumba, alisema alipochunguzwa, Bw Stephen Ongare alipatikana na ugonjwa wa ini unaohusishwa na upungufu wa maji mwilini na uliosababishwa na unywaji pombe haramu kupindukia.
Dkt Kipchumba alisema inashangaza, akiongeza kuwa maisha ya watu watatu hupotea kila mwezi katika mtaa wa mabanda wa Kayaba baada ya uchunguzi wa kitaalamu wa madaktari kubaini walevi waliozoea kunywa zaidi bila kula vizuri huuawa na pombe kali inayokausha maji mwilini.
“Ninaomba wasimamizi wa mitaa wakiwemo mkuu wa tarafa, machifu na manaifu wao na polisi wakaze kamba katika vita dhidi ya pombe haramu tusije tukapoteza kizazi kijacho,” Dkt Kipchumba alisema.
Kamanda wa polisi eneo la Makadara Bi Judith Nyongesa alithibitisha mwili huo ulipelekwa katika chumba cha kuhifadhi maiti cha City.