• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 8:55 PM
Drama washukiwa wa utekaji nyara wakinaswa

Drama washukiwa wa utekaji nyara wakinaswa

Na WAIKWA MAINA

MWAMUME na mpenziwe wanaohusishwa na utekaji nyara na kuteswa kwa mfanyabiashara wa Kamukunji, Nairobi, Bi Hafsa Mohamed Luqman, walikamatwa Kinangop, Kaunti ya Nyandarua, Jumapili.

Wawili hao walikamatwa katika Mkahawa wa Crystal katika kijiji cha Magumu na maafisa wa upelelezi wa jinai (DCI) nyakati za asubuhi katika operesheni iliyoendeshwa kisiri bila ufahamu wa raia, wakiwemo wasimamizi wa mkahawa huo maarufu.

Kulingana na mashahidi, maafisa wa DCI walikuwa na habari kwamba Bw Jackson Njogu, 24, na mpenzi wake Hafsa Abdiat, 21, wangelala katika mkahawa huo na ndipo wakawavizia.

Washukiwa hao waliwasili usiku wa manane na kukodi chumba cha kulala lakini wapelelezi waliwasili majira ya asubuhi wakijifanya kuwa wateja.

Isitoshe, Njogu na Abdiat walikuwa na nambari ya simu ya meneja wa hoteli hiyo na wakampigia simu wakiomba awatengee chumba cha kulala.

“Mwanamume mmoja alipiga nambari yangu ya simu ya mkono, akataja jina langu na kwa upole akaagiza chumba akisema ameandamana na msichana rafiki yake,” akasema Meneja wa Mkahawa huo wa Crystal, James Mwaura. Mwendo wa alfajiri meneja huyo alisema alishtuka alipoona kundi la wanaume saba ambao tayari walikuwa wameingia ndani ya majengo ya mkahawa huo.

Walifufuliza moja kwa moja hadi chumba ambako Bw Njogu na mpenzi wake walikuwa wamelala, wakavunja mlango, kuingia na kuwakamata washukiwa hao. Bw Mwaura aliwafuata maafisa hao katika chumba hicho akidhani walikuwa wahalifu, ila baadaye akang’amua kuwa walikuwa maafisa wa DCI.

“Hapakuwa na kelele wala patashika yoyote. Ni wateja waliokodi vyumba vya karibu waliosikia kilele hafifu na kilio cha mwanamke. Lakini maafisa hao waliwaomba wateja hao warejee katika vyumba vyao kwa upole wakiwahakikishia kwamba mambo yalikuwa shwari na kwamba maisha yao hayakuwa hatarini,” Bw Mwaura akaeleza.

Baada ya washukiwa hao wawili kukamatwa, walielekezwa nje ya mkahawa huo kulikokuwa na magari matatu aina ya Subaru, yaliyojaa maafisa wengine, yakiwasubiri.

Ilibainika kuwa maafisa hao, wote wanaume, ni wanachama wa kikosi cha Uchunguzi kuhusu Uhalifu na Masuala ya Ujasusi pamoja na maafisa wa kikosi cha kuwaandama wahalifu.

Wote, pamoja na maafisa wa DCI walikuwa wakiwaandama washukiwa hao wawili.

Inadaiwa kuwa Njogu na Bi Abdiat awali walikuwa wakibugia pombe katika baa iliyoko eneo lenye msitu kando ya barabara ya Magumu kwenda Thika.

Njogu alikuwa amevaa long’i na jaketi za jeans huku mwanadada huyo akiwa amevaa jaketi ya jeans yenye rangi ya kijivu uso wake ukiwa umefunikwa kwa leso, walipowasili katika mkahawa wa Crystal.

  • Tags

You can share this post!

JAMVI: Nassir atagundua siri ya kurithi joho la...

NI OGIER! Mfaransa Ogier atwaa ubingwa wa WRC Safari Rally