• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
Echesa akamatwe mara moja – Chebukati

Echesa akamatwe mara moja – Chebukati

MACHARIA MWANGI Na SAMMY WAWERU

MWENYEKITI wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Bw Wafula Chebukati amekashifu vikali tukio ambapo aliyekuwa Waziri wa Michezo, Rashid Echesa alionekana akimzaba kofi afisa mmoja wa tume hiyo eneo la Matungu, Kaunti ya Kakamega mapema Alhamisi.

Kwenye video, Bw Echesa alinaswa akimuangushia kofi afisa huyo wa IEBC kufuatia uchaguzi mdogo unaoendelea eneobunge hilo.

Tukio hilo lilitendeka katika kituo cha Shule ya Msingi ya Bulonga, wakati shughuli za kupiga kura zilikuwa zinaendelea.

Akizungumza baada ya kuzuru kituo cha kupigia kura cha Kiwanja Ndege, Naivasha, Bw Chebukati ameitaka idara ya polisi kumkamata mara moja waziri huyo wa zamani, huku akilaani tukio hilo.

“Uvamizi huo ni hatia, na ninaihimiza idara ya polisi kumtia nguvuni mhusika, achukuliwe hatua kisheria,” Bw Chebukati akaambia wanahabari.

Mwenyekiti huyo wa IEBC alisema chaguzi ndogo zinazoendelea maeneo kadha nchini ni za amani, ila matukio yaliyoshuhudiwa katika eneobunge la Matungu na Wadi ya London, Kaunti ya Nakuru.

Bw Chebukati alisema ni makosa kwa maajenti wa vyama kuzuru vituo tofauti vya kupigia kura kwa madai wanafuatilia shughuli ya upigaji kura.

Duru zinaarifu maafisa wa polisi wamezingira makazi ya Echesa yaliyoko eneo la Shibale, Mumias ya Kati, Kaunti ya Kakamega.

Idara ya polisi inahoji waziri huyo alihepa baada ya kumzaba afisa wa IEBC.

Kwenye video inayosambaa mitandaoni, Bw Echesa anaskika akitaka kuelezwa kwa nini maajenti wa chama cha UDA na ambacho kinahusishwa na Naibu wa Rais, Dkt William Ruto, walifurushwa kwenye kituo cha kura.

Katika ziara yake Naivasha, Bw Chebukati alisisitiza kwamba IEBC imejitolea kuhakikisha chaguzi ndogo zinazoendelea maeneo tofauti nchini ni za huru, haki na uwazi.

Mbali na visa vya Matungu – Kakamega na London – Nakuru, Bw Chebukati alisema hakujaripotiwa matukio yenye uzito.

Aliwataka maafisa wa IEBC kuhakikisha sheria na mikakati iliyowekwa kuzuia msambao wa ugonjwa wa Covid-19 zinatiliwa mkazo.

You can share this post!

Wabunge 4 wa Tangatanga wakamatwa kwa kuhonga wapigakura

Malala alia kuna wizi wa kura Matungu