• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 10:48 AM
Wabunge 4 wa Tangatanga wakamatwa kwa kuhonga wapigakura

Wabunge 4 wa Tangatanga wakamatwa kwa kuhonga wapigakura

 JARED NYATAYA na CHARLES WASONGA

WABUNGE wanne wa mrengo wa Tangatanga wangali wanazuiliwa katika kituo cha polisi cha Bungoma baada ya kukamatwa kwa madai ya kuwahonga wapiga kura katika uchaguzi mdogo unaoendelea eneo bunge la Kabuchai.

Didmus Barasa (Kimilili), Nelson Koech (Belgut), Wilson Kogo (Chesumei) na seneta wa Nandi Samson Cherargei walikamatwa Alhamisi asubuhi katika eneo la Masese, Kaunti ya Bungoma. Eneo hilo liko karibu na barabara ya kutoka mjini Chwele- Bungoma.

“Hatujaachiliwa. Bado tumezuiliwa hapo na bila kuambia makosa yetu. Inaonekana kuwa serikali inapanga kuendeleza wizi wa kura kwa sababu sisi ni maajenti wa mgombeaji wetu. Hakuna ushahidi kuwa tulikuwa tukiwahonga wapiga kura, inavyodaiwa,” Bw Barasa akaambia Taifa Leo kupitia ujumbe mfupi.

Sasa chache kabla ya shughuli ya kupiga kura kuanza viongozi wa Ford Kenya wakiongozwa na kinara wao Moses Wetang’ula na mgombeaji wa chama hicho Joseph Majimbo, walilalamika kuwa wandani hao wa Naibu Rais William Ruto walikuwa wakiwahonga wapiga kura.

Bw Majimbo pia alielekeza kidole cha lawama kwa wabunge wengine wa Tangatanga John Waluke (Sirisia) na Fred Kapondi (Mt Elgon) kwa kutoa vishawishi vya fedha kwa wananchi ili wampigie kura mgombeaji wa United Democratic Alliance (UDA) Evan Kakai.

“Tunataka maafisa wa polisi na wale wa IEBC kufanya uchunguzi wa kina kuhusu visa hivi vya utoaji hongo kwa wapiga kura. Uamuzi wa wananchi unapasa kuheshimiwa katika uchaguzi huu,” Bw Wetang’ula akawaambia wanahabari.

Hata hivyo Bw Kakai alikana madai hayo na badala yake akaisuta Ford Kenya kubuni madai hayo na kuchochea fujo.

“Wameamua kushiriki fujo na propaganda zisizo na maana yoyote. Hii inaonyesha kuwa Ford Kenya wameingiwa woga,” mgombeaji huyo wa UDA akasema baada ya kupiga kuta katika Shule ya Msingi ya Pongola.

You can share this post!

Mwaniaji wa udiwani wa UDA akamatwa kwa kuhonga wapigakura

Echesa akamatwe mara moja – Chebukati