Na MASHIRIKA
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO
ANTOINE Griezmann alifunga bao naye Olivier Giroud akapachika wavuni magoli mawili katika ushindi wa 3-0 uliosajiliwa na timu ya taifa ya Ufaransa dhidi ya Bulgaria mnamo Juni 8, 2021.
Ufaransa ambao ni mabingwa wa dunia walipanga kikosi cha wanasoka wazoefu huku Kylian Mbappe, Karim Benzema na Griezmann wakiongoza safu ya mashambulizi.
Griezmann aliwafungulia Ufaransa ukurasa wa mabao katika dakika ya 29 kabla ya Giroud kutokea benchi na kufunga magoli mawili ya haraka katika dakika za 83 na 90.
Ufaransa wameratibiwa kuanza kampeni zao za Kundi F kwenye Euro kwa kupepetana na Ujerumani mnamo Juni 15 kabla ya kumenyana na Hungary mnamo Juni 19 kisha mabingwa watetezi Ureno mnamo Juni 23.