Na KALUME KAZUNGU
GAVANA wa Machakos, Dkt Alfred Mutua, amedai kuwa uongozi mbaya ndio uliosababisha hitaji la kuwepo kwa muafaka kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kiongozi wa ODM Raila Odinga, almaarufu handisheki.
Kiongozi huyo wa Chama cha Maendeleo Chap Chap alisema nchi tajiri, zenye rasilimali na zinazochunga masilahi ya wananchi wake huwa hazihitaji masuala kama handisheki na Mpango wa Maridhiano (BBI).
Kulingana naye, BBI na handisheki zilisababishwa na hitaji la kukomboa mwananchi wa Kenya dhidi ya maisha magumu ya kiuchumi.Akizungumza katika ziara eneo la Mpeketoni, Kaunti ya Lamu, Dkt Mutua aliwasisitizia viongozi wenzake kuhakikisha kuwa kadri wanavyopigania masuala ya kisiasa, ni vyema pia wahakikishe raia anazingatiwa kimaisha.
“Huwezi kuishi katika nchi ambayo unalala njaa kila wakati mpaka kufa kwako kama inavyofanyika Kenya kwa sasa. Nitakapokuwa rais nataka nchi ambayo huku tukifuata siasa, pia tuangazie mambo ya kuongeza pesa katika mifuko ya watu wetu. Watu wakishiba hawatapigana,” akasema.
Handisheki ilitokea mwaka wa 2018 baada ya Bw Odinga kula kiapo katika uwanja wa Uhuru Park kuwa ‘rais wa wananchi’ kufuatia uchaguzi uliosbabaisha mgawanyiko mkubwa nchini ambapo Rais Kenyatta ndiye alitangazwa mshindi wa urais katika awamu ya pili ya uchaguzi 2017.
Alisema wakati umewadia kwa wakenya kuchagua viongozi ambao watajali masuala ya kimsingi ya wananchi wao.“Tofauti za kimatabaka, hasa kati ya matajiri na maskini zinaletwa na uongozi mbaya. Kila wakati utasikia vita na manung’uniko kutoka kwa maskini, hali ambayo huwezi ukaishuhudia kwa matajiri.
Lazima tuvunje hizi tofauti na migawanyiko ya kimatabaka kwa kuhakikisha kila mwananchi yuko na pa kujipatia riziki, pesa, yuko na miundomsingi bora bila kujali amezaliwa au anaishi wapi. Ni haki ya kila mmoja wetu kupata mahitaji ya kimsingi,” akasema Bw Mutua.
Bw Mutua ni mmoja wa wanasiasa ambao tayari wametangaza nia ya kuwania urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka ujao.