NA MWANDISHI WETU
NAIBU Rais Rigathi Gachagua amerauka asubuhi na mapema kutembea mjini Kakamega akipata fursa ya kipekee kujionea wakazi wakiendelea na shughuli zao za wikendi.
“Hii asubuhi nimejionea mandhari ya kuvutia katika mji wa Kakamega,” ameandika Naibu Rais kwenye ukurasa wake wa mtandao wa Twitter.
Amesema amepunga hewa safi kutokana na upekee wa miti mingi na misitu muhimu katika kipindi hiki ambapo dunia inakabiliwa na matatizo ya mabadiliko ya tabianchi.
Bw Gachagua amesema miti mjini Kakamega na viungani mwa mji huo ni kitulizo kamili kwa wenyeji na wageni wanaozuru Magharibi mwa Kenya.
Baadaye Bw Gachagua ameungana na Rais William Ruto aliyehudhuria maombi ya muungano wa makanisa mbalimbali katika uwanja mdogo wa ndege ulioko katika kaunti jirani ya Bungoma.
Rais Ruto anafanya ziara katika eneo la Magharibi kutangamana na wakazi, ambao wengi ni wa jamii ya ‘Mulembe’.