NA SAMMY WAWERU
MBUNGE wa Kimilili, Didmus Barasa amezua ucheshi akidai kiongozi wa upinzani, Raila Odinga anapaswa kuwekewa simba mlangoni ili kuzuia jitihada zake kuendelea kukosoa matokeo ya urais 2022.
Akizungumza Jumapili, Agosti 27, 2023 katika hafla ya pamoja ya maombi Bungoma iliyoongozwa na Rais William Ruto, mbunge huyo alisema Kenya Kwanza ilipaswa kuwekea Bw Raila vikwazo vikali baada ya kumbwaga katika uchaguzi mkuu Agosti 9, 2023.
Dkt Ruto yuko ziara ya siku tano Eneo la Magharibi, ambapo anatarajiwa kuzindua miradi mbalimbali ya maendeleo.
“Raila Odinga tulipompeleka Bondo 2022 kwa wilibaro, tulipaswa kumuwekea simba mlangoni asiwe anatoka,” Bw Barasa alisema.
Kauli ya mbunge huyo ambaye ni mwandani wa Rais Ruto, ililenga hatua ya Bw Raila kuendelea kupinga uhalisia wa serikali ya Kenya Kwanza.
Waziri Mkuu huyo wa zamani, alimenyana na Dkt Ruto 2022 kuingia Ikulu, kupitia tikiti ya Azimio la Umoja.
Raila alipeperusha bendera ya Azimio akisaidiwa na Bi Martha Karua, kama mgombea mwenza, naye Ruto (Kenya Kwanza) akisaidiwa na Bw Rigathi Gachagua ambaye kwa sasa ndiye Naibu Rais.