• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 5:50 AM
Kampuni za ndege Afrika zakumbatia teknolojia ya paspoti za kidijitali kuokoa biashara

Kampuni za ndege Afrika zakumbatia teknolojia ya paspoti za kidijitali kuokoa biashara

NA RICHARD MAOSI

KAMPUNI za ndege za Afrika zimeanza kukumbatia teknolojia ya Umoja wa Afrika (AU) ya kuwapa abiria paspoti za kidijitali kurahisisha usafiri.

Kampuni za Kenya Airways na Ethiopian Airlines zimeungana na Shirikisho la Usafiri wa Angani Afrika Magharibi na Kati (ASKY) kutumia mtandao wa PANABios unaoendeshwa na AU ikishirikiana na Vituo vya Kuzuia Magonjwa Afrika (Africa CDC).

Bw Justus Thairu, afisa wa mauzo wa Kenya Airways alisema jukwaa hilo la kidijitali kwa jina Trusted Travel Pass litawezesha abiria kuthibitisha vipimo vyao na vyeti vya corona kwa haraka kabla ya kupanda ndege.

“Tunafurahia kushirikiana na AU na Africa CDC katika jitihada zao za kuhakikishia abiria usalama wa kiafya huku pia maambukizi mipakani yakipunguzwa,” alisema.

Akihutubu alipozindua matumizi ya teknolojia hiyo, afisa wa mawasiliano katika kampuni ya Ethiopian Airlines alisema ubunifu huo utasaidia kampuni hiyo kuongoza mapato katika kipindi hiki kigumu cha biashara.

“Wateja wa Ethiopian Airlines sasa wataweza kufurahia safari za angani bila bughudha wakitumia paspoti za kidijitali. Zitawawezesha maafisa katika viwanja vya ndege kutambua iwapo abiria wamechanjwa na kama wametimiza masharti ya kudhibiti virusi vya corona,” alisema kwenye taarifa iliyoonekana na Taifa Leo ilisema.

ASKY ilisema imependezwa na juhudi za AU kwa kuhakikisha bara la Afrika lina mtandao wake wa kuthibitisha vipimo vya corona kupitia kwa maabara, hali ambayo inahakikisha biashara inaendelea kama kawaida miongoni mwa mataifa ya Afrika.

“Tukishirikiana na AU, tunaunda mfumo wa Kiafrika wa kiwango cha kimataifa unaowajali Waafrika wote bila ubaguzi na kutokomeza ufisadi katika sekta ya afya, huku ukipunguza gharama ya vipimo vya maabara. Pia utatusaidi kukusanya data yetu kutuwezesha kufanya maamuzi haraka,” ikasema ASKY kwenye taarifa.

Mfumo huo wa PANABios unatarajiwa kuboresha usimamizi wa sera kote Afrika na kuinua biashara baina ya mataifa, kupiga jeki utalii, uwekezaji na utamaduni, na hatimaye kuhakikisha Afrika haiachwi nyuma na mabara mengine katika maendeleo.

“ASKY inaona faraja kwa AU kutengeneza na kuzindua mradi huu kabla ya mabara mengine, na kuyapa mataifa ya Afrika Imani ya kufungua uchumi kwa kumshirikisha kila mwananchi,” akasema Bw Ahadu Simachew, afisa mkuu mtendaji wa ASKY.

Dkt John Nkengasong, mkurugenzi wa Africa CDC alisema ushirikiano na kampuni za ndege utakuwa nguzo muhimu katika kuokoa biashara zilizoangushwa na corona.

“Kiwango cha madhara yaliyoletwa na Covid-19 kinahitaji ushirikiano mkuu na ubunifu wa kiteknolojia. Kutumika kwa teknolojia yetu kutasaidia pakuwa kunyanyua maazimio yetu ya maendeleo kama bara,” alisema.

You can share this post!

Faida za pilipili mboga

Kenya kunufaika na kuchaguliwa kwa Maluki kuwa mwenyekiti...