NA ALEX KALAMA
WAZIRI wa Usalama wa Ndani nchini Prof Kithure Kindiki leo Jumanne amefika katika msitu wa Shakahola ambapo zaidi ya miili 90 imegunduliwa kuzikwa kwenye makaburi yenye kina cha urefu wa futi mbili.
Waziri huyo alikuwa ameandamana na mshirikishi wa Pwani Rhoda Onyancha.
Amesema kuwa serikali itaunda timu ya kuhusisha asasi na vitengo mbalimbali (mult-agency team) ili kuhakikisha kuwa operesheni inaendeshwa kisawasawa na hata kuokoa watu zaidi.
“Tunalaani vikali unyama uliotekelezwa hapa Shakahola na tunaomba mahakama ifanye kazi yake kwa bidii wakati mwafaka ukifika na kuwaweka wahusika wa maovu yaliyotendeka hapa mbele ya sheria,” amesema Prof Kindiki.
Kindiki alikuwa Shakahola ili kujionea jinsi ambavyo operesheni ya kuwaokoa manusura wa dhehebu la mchungaji Paul Mackenzie inavyoendeshwa pamoja na ufukuaji wa miili ya waathiriwa wa mafunzo potovu.
Mhubiri Mackenzie kwa sasa amezuiliwa na polisi.
Aidha waziri huyo amemfananisha mhubiri huyo na gaidi hivyo basi akasema serikali itafanya kila iwezalo kuhakikisha kwamba wale wote ambao wamekuwa wakishirikiana na Mackenzie kutekeleza maovu hayo watakabiliwa kisheria.
Kindiki ameeleza kuwa dini ni kitu kitakatifu na haipaswi kutumiwa kuendeleza shughuli za kigaidi za kuua watu wasio na hatia eti ndipo wakutane na Yesu na kuurithi ufalme wa mbinguni.