• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 6:39 PM
Mbunge aitaka serikali ijenge shule zilizozama

Mbunge aitaka serikali ijenge shule zilizozama

Na FLORAH KOECH

MBUNGE wa Baringo Kusini Charles Kamuren ameitaka serikali itoe pesa za ujenzi wa shule sita mpya ambazo zilisombwa na maji ya mafuriko mwaka 2020.

Shule hizo zilisombwa baada ya Mto Baringo kuvunja kingo zake na sasa zitajengwa upya katika ardhi nyingine ambayo ishatolewa na jamii ya eneo hilo kwa hiari.

Kando na shule, vituo vya kiafya, masoko, makanisa na makazi ya zaidi ya watu 10,000 pia yalisombwa na maji.

Zaidi ya shule 15 ziliathiriwa na mafuriko hayo na sasa wanafunzi kutoka shule hizo wamejiunga na wenzao kutoka shule jirani.

Kati ya shule za upili zilizosombwa ni Salabani, Ng’ambo Girls’ na shule ya mseto ya Lake Baringo. Shule za msingi za Ng’ambo, Sintaan, Leswa, Lorok,Loruk, Loropil, Noosukro, Kiserian, Loruk,Ilng’arua, Ng’enyin, Sokotei na Salabani pia zilisombwa na maji hayo ya mafuriko.

Shule hizo zilifaa kujengwa upya na serikali lakini hadi sasa bado hilo halijafanyika huku Bw Kamuren akisema kwamba shughuli za masomo zinaendelea kutatizika.

Bw Kamuren alisema hali itakuwa mbaya mno wanafunzi wa kidato cha kwanza wakitarajiwa kuripoti shuleni mnamo Julai.

“Naomba serikali itoe fedha kwa ujenzi upya wa shule zilizosombwa na maji ya mafuriko. Kwa sasa wanafunzi wanasomea mazingira magumu na hali itakuwa mbaya zaidi wakati wanafunzi wa kidato cha kwanza wataripoti shuleni,” akasema Bw Kamuren.

Kwa mujibu wa mwanasiasa huyo serikali iliahidi kutoa Sh10 milioni kwa ujenzi wa shule za upili na Sh5 milioni kwa ujenzi wa shule za msingi.

“Bado hatujapata fedha zozote kutoka kwa serikali mwaka moja baada ya ahadi hiyo kutolewa. Tumetumia pesa kidogo kutoka kwa Hazina ya Maeneobunge (NG-CDF) kujenga madarasa machache. Wanafunzi wetu hawawezi kuendelea kusomea chini ya miti,” akaongeza Bw Kamuren.

Taifa Leo ilibaini kwamba vyandarua ambavyo vilikuwa vimetolewa na Shirika la Msalaba Mwekundu sasa vimeraruka na havisaidii sana kuwakinga dhidi ya mvua na jua kali.

Kamishina wa Kaunti ya Baringo Henry Wafula alithibitisha kwamba pesa za kujenga upya shule hizo zinatolewa hivi karibuni.

“Serikali bado ilikuwa kutathmini hali na kukadiria gharama ya ujenzi. Pesa hizo zitatolewa hivi karibuni ila kwa sasa wanafunzi wanaweza kuendelea kusomea katika shule jirani,” akasema Bw Wafula.

You can share this post!

Saint George Ethiopia, Wakenya watakia Matasi afueni baada...

WHO yatoa majina mapya kurejelea virusi vya corona