Na Maureen Ongala
MBUNGE wa Ganze, Bw Teddy Mwambire, amewataka maafisa wa polisi waanzishe uchunguzi kuhusu vijana wanaosemekana kubaka akina mama wazee katika Kaunti ya Kilifi.
Kulingana na Bw Mwambire, kumekuwa na malalamishi ya visa hivyo huku waathiriwa wengi wakiwa ni wajane wakongwe wasiojiweza.
“Tunashuku kuwa vijana hawa ni wahuni ambao hutumia mihadarati na wameshindwa kutongoza wasichana,” akasema.
Mbunge huyo alisema waathiriwa huwa hawaripoti kwa polisi unyama wanaofanyiwa kwa vile wanahofia unyanyapaa kutoka kwa jamii.
“Kwa sababu ya umri wao, waathiriwa hawajui kuwa ni lazima waripoti visa hivi katika vituo vya polisi, na kwamba pia wana haki ya kutafuta haki kwa ukatili a waliofanyiwa kupita korti,” akaeleza.
Mbunge huyo alisema maeneo yaliyoathirika mno ni Vitengeni, Malanga na Wacho katika wadi ya Bamba.
Aliongeza kuwa wazee hao pia wanahitajika kuhamisishwa jinsi ya kutunza ushahidi ili kufanikisha kesi zao kortini.
Amewataka maafisa wa polisi kuwashughulikia waathiriwa na heshima ndipo wawaondolee hofu ya kudhulumiwa zaidi endapo wataamua kupiga ripoti.
Visa hivyo vinazidi kuhatarisha maisha ya wakongwe ambao tayari huishi kwa hofu ya kuuliwa kwa madai kuwa ni wachawi kwa sababu ya mvi.