NA WINNIE ONYANDO
MKE wa Naibu Rais Rigathi Gachagua, Dorcas Rigathi, sasa anasisitiza kuwa serikali haina uwezo wala mamlaka ya kudhibiti makanisa.
Akihutubia Ushirika wa Wachungaji wa Kiambu katika kongamano la makasisi katika Kanisa la Christian Church International (CCI) mjini Thika, Kaunti ya Kiambu mnamo Jumanne jioni, Bi Dorcas alishikilia kuwa kudhibiti makanisa ni sawa na kuwanyima waumini uhuru wa kuabudu kama inavyopendekezwa katika Katiba ya Kenya.
Mchungaji Dorcas alisisitiza kwamba makanisa ni vuguvugu la kiroho ambalo linafanya kazi kwa misingi ya imani kama dira ya maadili na dhamiri ya jamii.
Kwa hivyo, alishikilia kuwa serikali haina uwezo wa kudhibiti mienendo ya kiroho kwani haina ufahamu kuhusu masuala ya kiroho.
“Huwezi kutunga sheria ya kudhibiti kile ambacho hukielewi. Wanaposema kanisa litawaliwe na mtu aliye na masomo ya juu kama vile digrii na shahada ya uzamifu, basi haitawezekana. Kadhalika hilo haliko kwenye Biblia,” akasema Bi Dorcas.