• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 5:50 AM
Mume wangu hana ustadi wa kucheza mechi chumbani, nifanyeje?

Mume wangu hana ustadi wa kucheza mechi chumbani, nifanyeje?

Nimeolewa kwa miezi kadhaa. Tulikubaliana na mchumba wangu kwamba hatutaonja asali hadi tutakapooana. Sasa nimegundua ni mbichi sana katika masuala ya chumbani. Nifanye nini?

Sielewi unatarajia mume wako atoe wapi ujuzi wa mambo hayo ilhali ulimwambia msubiri hadi ndoa. Kama una ujuzi, usione aibu kumfunza jinsi ya kukupa raha. Kama huna, shirikiana naye mjifunze.

Nimemwacha sababu ananishuku kila mara

Nimemuacha mpenzi wangu baada ya kugombana mara kadhaa akidai mimi si mwaminifu kwake. Nampenda kwa dhati na sina mwingine. Naomba ushauri wako.

Mpenzi wako anasumbuliwa na wivu. Mapenzi yanahitaji mtu kujiamini ndipo aweze kumwamini mwenzake. Wivu hutokana na hali ya mtu kutojiamini. Ushauri wangu ni kwamba umpe muda uone kama atabadilika na akishindwa uachane naye uendelee na maisha yako.

Anapenda starehe na pesa licha ya kuwa na mtoto, nimechoka!

Nimependana na mwanamke aliye na mtoto. Lakini mapenzi yake yananishinda. Anapenda maisha ya starehe na sina pesa. Sasa anatishia kuniacha. Nifanye nini?

Mapenzi ya dhati hayana masharti. Kwa kutishia kukuacha, mpenzi wako amethibitisha kuwa anahitaji mwanamume mwenye uwezo wa kugharamia mahitaji yake ya pesa. Kama huna uwezo huo achana naye.

Mpenzi wangu ni mrembo sana lakini bado natamani wengine

Mpenzi wangu ni mrembo sana, wanaume wengi wakimuona hudondokwa na mate wakimtamani. Ajabu kuwa nikiona wanawake wengine bado nawatamani. Ni kwa nini?

Aliyesema binadamu hatosheki hakukosea. Hata hivyo, amepewa uwezo wa kujizuia kuongozwa na tamaa. Unaungama kuwa umebahatika kupata mpenzi anayekufaa. Tulia kwake na umpe moyo wako wote.

  • Imeandaliwa na Fatuma Bariki

  • Tags

You can share this post!

Machozi kwa Senegal, Ghana na Cameroon katika vita vya...

Hamiliki nyumba wala shamba Nairobi, lakini anazalisha...

T L