• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
Mwanamke atoroka mumewe na kuolewa na ‘roho mtakatifu’

Mwanamke atoroka mumewe na kuolewa na ‘roho mtakatifu’

Na OSCAR KAKAI

MWANAMKE wa umri wa miaka 41 ameshangaza mumewe pamoja na wakazi wa mji wa Makutano, Pokot Magharibi, baada ya kutangaza kuwa ameolewa na roho mtakatifu.

Elizabeth Nalem ambaye ni afisa wa kaunti mjini hapo aliandaa sherehe ya kufunga ndoa na roho mtakatifu katika hafla iliyoandaliwa kwenye hoteli ya Chelang’a mjini Makutano.

Bi Nalem aliandamana na wafanyakazi wenzake wa kaunti pamoja na wafanyabiashara wa kike katika hafla hiyo ambapo alikula kiapo cha kuwa mwaminifu kwa ‘mumewe’ mpya – roho mtakatifu.

Bi harusi alikuwa amevalia mavazi ya harusi na sherehe ilipambwa kwa vigelegele kutoka kwa akina mama huku mumewe, Joshua Nalem, akifuatilia tukio hilo kwa mshangao.

Sherehe hiyo iliongozwa na Kasisi Albert Rumaita wa kanisa la Full Gospel.

“Nimetumikia dunia tangu nilipozaliwa. Lakini sasa roho mtakatifu ameniagiza nitumikie Mungu. Roho Mtakatifu alinituma kwa Pasta Rumaita ambaye alininunulia vazi la harusi, aliandaa hafla hii na akakodisha magari yaliyotuleta haba,” akasema Bi Nalem ambaye ni mama ya watoto sita.

Alisema kwamba kabla ya kuandaa hafla hiyo aliomba ruhusa kwa mumewe, lakini ombi lake likakataliwa.

Jumanne, Bw Nalem aliyeonekana kupigwa na butwaa alishuhudia mkewe ambaye wameishi pamoja kwa miaka 20, akiapa kumpenda na kutoa maisha yake kwa ‘mume’ mwingine asiyeonekana.

“Nimeshangaa sana. Nilitoa mahari; ng’ombe 22 na mbuzi 15 nilipooa mke wangu. Lakini sasa anafunga ndoa na mume mwingine anayedai kuwa roho mtakatifu,” akasema.

Bw Nalem alifichua kuwa ndoa yao imekuwa ikikumbwa na msukosuko kwa miezi kadhaa.

Alisema mvutano baina yao ulianza baada ya mkewe kuanza kubadili mwenendo wake wa maombi.

“Alianza kuamka usiku wa manane kuomba na kila mara nilipomuuliza alikimbia kwa jirani na kuniacha peke yangu,” akasema Bw Nalem.

You can share this post!

Presha Raila amlipe Ruto deni la kisiasa

Korti yacharaza Uhuru kiboko mara nyingine ikisema alipuuza...