Na Wycliffe Nyaberi
MWANAMUME katika soko la Riosiri, eneobunge la Mugirango Kusini, Kaunti ya Kisii, amemshtaki mbunge wa zamani wa eneo hilo Bw Omingo Magara, akitaka amtambue kuwa mwanawe.
Bw Justus Arunga Mauti, 39, anadai kuwa kiongozi huyo wa chama cha Peoples Democratic party (PDP) ndiye babake aliyemzaa na hivyo basi anafaa kutambuliwa na kuonyeshwa upendo kama watoto wengine wa Bw Magara.
Mlalamishi ni mfanyabiashara aliye na duka ndogo ambalo amelitaja ‘Mwanaharamu Usiseme Kitu’.
Kupitia kwa wakili wake, jamaa huyo anaiomba mahakama imshurutishe Bw Magara akubali wafanyiwe uchunguzi wa DNA ili kuthibitisha ikiwa wana uhusiano wowote au la.
Bw Magara, kupitia kwa wakili, anaitaka mahakama itupilie mbali kesi hiyo akidai mlalamishi anadanganya.
Kulingana naye, alimfahamu mamake Bw Mauti kama mke wa diwani ambaye alikuwa rafiki yake kisiasa ambaye alishafariki na hangemkosea heshima kwa kiasi hicho.