Mwili wa mwanamume wapatikana kwenye tanuri la uchomaji makaa
Na MWANGI MUIRURI
Mwili wa mwanamume katika Kaunti ya Murang’a umepatikana ukiwa ndani ya gunia na ukiwa juu ya tanuri la uchomaji makaa.
Kisa hicho cha Kijiji cha Ndutumi kilichoko eneo bunge la Kiharu kimewaacha wengi vinywa wazi ikizingatiwa kuwa mwanamume huyo alitambuliwa kama mchomaji makaa.
Kamanda wa polisi wa Kaunti ya Murang’a Bw Mathiu Kainga alisema kwamba uchunguzi umeanza kuhusu suala hilo.
“Hiki ni kitendawili cha kweli lakini maafisa wetu watakitegua tu. Mwili umechukuliwa na kupelekwa katika mochari ya Kaunti kungojea upasuaji ili tubaini mazingara halisi ya mauti hayo,” akasema.
Maswali ambayo wapelelezi waliofika eneo hilo kuchunguza alikopatikana mwanamume hayo yaliorodheshwa kuwa matano.
1. Aliuawa kwingine akatupwa hapa?
2. Alijiweka kwa gunia ndio alale juu ya tanuri hili lenye joto lakini moshi hatari wa makaa ukamuua?
3. Alikuwa akilenga kujitoa uhai akitumia hewa sumu ya makaa?
4. Aliuawa katika eneo hilo la makaa katika kisasi cha kibiashara?
5. Uwezekano mwingine wowote.
Maafisa hao walisema upasuaji wa maiti utaupa uchunguzi taswira na mashiko kwa kuwa utaonyesha iwapo aliuawa.
Next article
Mwanamume ashtakiwa kuhusisha Jenerali Ogolla na maandamano...