• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 2:24 PM
Njeri Maina aambiwa angetafuta matibabu hospitali ya Kerugoya kufuatia shambulizi

Njeri Maina aambiwa angetafuta matibabu hospitali ya Kerugoya kufuatia shambulizi

Na MWANDISHI WETU

MASWALI yameibuka kwa nini Mwakilishi wa Kike katika Kaunti ya Kirinyaga Njeri Maina alisafirishwa Nairobi kwa matibabu ilhali kuna hospitali ya hadhi ya juu ya Kerugoya iliyofunguliwa majuzi.

Hospitali hiyo ya rufaa ilifunguliwa na Rais William Ruto akiandamwa na Naibu wake Rigathi Gachagua mnamo Juni. Wakiipigia debe hospitali hiyo, Rais Ruto alisema kuwa itawanufaisha wakazi wa eneo hilo.

Hata hivyo, wanamitandao walitia dukuduku wakati Bi Maina alisafirishwa hadi jijini Nairobi kwa matibabu kufuatia tukio ambapo alishambuliwa na watu wasiojulikana.

Inasemekana kuwa Bi Maina alipata majeraha ya kichwa ndiposa alisafirishwa mpaka Nairobi huku akilazimika kunyolewa nywele ili kutathminiwa na madaktari.

Wafuasi wa Bi Maina wamemhusisha gavana wa kaunti hiyo Anne Waiguru na kipigo hicho huku wakirai serikali imkamate. Ni jambo ambalo gavana huyo anakanusha vikali kupitia taarifa yake huku akirai polisi kuchukua hatua.

“Nimepata ujumbe kupitia vyombo vya habari kuwa Mwakilishi wa Wanawake katika kaunti ya Kirinyaga Njeri Maina ameshambuliwa na vijana alipokuwa akielekea katika stesheni ya polisi ili kujibu wito wao. Ningependa kulaani matendo hayo ya vita na nisisitize kuwa hatutakubali wala kuvumilia vita,” akaandika kwenye akaunti yake ya Facebook.

Vurugu zilizuka baada ya Bi Maina kufika katika kituo cha polisi cha Kerugoya kurekodi kauli yake kuhusiana na kuharibiwa kwa kisima cha maji kinachotumia jua.

Bi Maina anatuhumiwa kuwashawishi vijana kuharibu mradi huo baada ya wakazi wa eneo hilo la Kanyekini kutoruhusiwa kutumia kisima hicho.

Baada ya kuandikisha kauli yake, Bi Maina ambaye alikuwa ameandamwa na mjumbe wa wadi ya Baragwi David Mathenge, alisema kuwa angemwakilisha Bw Mathenge iwapo angepelekwa kortini.

“Mathenge hakuwa amekosa hata sababu nilikuwa napatiana cheki za benki kwa kikundi cha wanawake nilipoulizwa na wakazi wa Mukandu-ini kwa nini mradi huo umechukua muda mwingi na ni tu mtu mmoja ananufaika na maji ya kisima hicho,” akasema.

 

  • Tags

You can share this post!

Fahamu kwa nini wanaume Lamu wanapenda kula hotelini kuliko...

Ripoti zasema Yevgeny Prigozhin wa Wagner ameangamia

T L