• Nairobi
  • Last Updated May 11th, 2024 11:02 AM
Padri wa Kanisa la Katoliki apatikana ameaga dunia kwenye lojing’i Murang’a baada ya kukesha na kipusa wakijivinjari

Padri wa Kanisa la Katoliki apatikana ameaga dunia kwenye lojing’i Murang’a baada ya kukesha na kipusa wakijivinjari

NA MWANGI MUIRURI

PADRI wa Kanisa la Katoliki alipatikana amefariki Jumamosi, Julai 8, 2023 kwenye lojing’i Murang’a, ambapo inasemekana alikuwa akijivinjari na mwanamke mwenye umri wa miaka 32.

Ripoti ya polisi iliyonakili kisa hicho, ilifichua kwamba Padri Joseph Kariuki, 43, wa Parokia ya Ruai, Kaunti ya Nairobi aliingia katika Mkahawa wa Monalisa ulioko katika eneobunge la Gatanga mnamo Ijumaa jioni, akiandamana na kibarafu wake wa moyo na wakakodisha chumba cha malazi.

Kisha, waliagiza mvinyo na mapochopocho ambapo baada ya kujipa raha ya shibe na kukata kiu, waliingia chumbani kupiga moyo pasi.

“Lakini asubuhi ya saa mbili kidosho alishuhudia padri akisinzia kama aliyeduwaa na pia kuishiwa na uhai. Alikimbia kuita wasimamizi wa hoteli ambao walikimbia katika chumba na harakati za kumpeleka padri hospitalini zikaanza,” ripoti ya polisi inaelezea.

Wasimamizi wa hoteli hiyo aidha walipiga simu kwa kituo cha polisi cha Samura, ambapo maafisa wawili walitumwa kuwajibikia mwito.

“Maafisa waliofika walipata padri akiwa ameondolewa chumba cha kulala na kuwekwa katika gari lake aina ya Toyota Harrier la rangi nyeusi na uchi wake ukiwa umefunikwa kwa shuka la kitanda,” afisa mkuu wa polisi wa Gatanga Bw Laurence Njeru akasema.

Maafisa hao wa polisi wakiandamana na wafanyakazi wawili wa hoteli na pia kidosho wa padri walipeleka mgonjwa hadi hospitali ya Kenol ambapo alibainishwa kuwa alikuwa ameaga dunia.

Mwili ulisafirishwa hadi mochari ya Mater iliyokojijini Nairobi, huku polisi wakisema mauti hayo yanachunguzwa kupitia taarifa za mashahidi na pia uchunguzi wa kimaabara.

Bw Njeru alisema kwamba chembechembe za mvinyo na chakula ambacho wapenzi hao wawili walitumia zimechukuliwa kwa uchunguzi zaidi, huku upasuaji wa mwili ukitarajiwa kutoa taswira kamili kuhusu mauti hayo.

 

[email protected]

 

 

  • Tags

You can share this post!

Mume na mke watambuliwa kortini kama wavamizi wa mkurugenzi...

Mwanamuziki John Njagi anavyolima mahasidi wake kwa cheche...

T L