• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 11:53 AM
Polisi wagundua waliyemsaidia kupata matibabu ni jambazi sugu

Polisi wagundua waliyemsaidia kupata matibabu ni jambazi sugu

NA MWANGI MUIRURI

MWANAMUME aliyepigwa risasi katika mji wa Thika, ambaye polisi walisaidia kupata matibabu Jumanne usiku, aligeuka kuwa mshukiwa wa ujambazi aliyejihami kwa silaha, ambaye sasa yuko chini ya ulinzi wa polisi akiendelea kupona kabla ya kukabiliana na mkono wa sheria.

Maelezo kumhusu mwanamume huyo yaliwaongoza wapelelezi hadi kwenye nyumba yake katika mtaa wa Makongeni ambapo bastola aina ya Ceska iliyokuwa na risasi 15 iliyofichwa chini ya mkeka ilipatikana.

Polisi pia walisema walipata misokoto ya bangi ndani ya nyumba hiyo. Polisi sasa wanaamini kuwa mwanamume huyo aliyelazwa katika hospitali ya Thika Level Five anahusishwa na visa vya wizi wa kutumia silaha katika Kaunti za Nairobi na Kiambu.

Shida kwa mwanamume huyo ilianza baada ya kufyatuliwa risasi na mtu aliyekuwa ndani ya gari la kibinafsi ambaye baadaye aliondoka kwa kasi na kumwacha akiwa amejeruhiwa na kuvuja damu.

“Tukio hilo lilikuwa karibu na hospitali yenyewe. Tulimkuta mtu aliyejeruhiwa vibaya ambaye tulimsaidia hospitalini akivuja damu kwa wingi,” maafisa wa polisi walisema kupitia mawasiliano rasmi ya polisi.

Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) iliongeza kuwa bunduki iliyopatikana nyumbani kwa mwanamume huyo ilipokonywa mtu aliyekuwa na leseni ya kuimiliki huko Kahawa Sukari mnamo Januari 28, 2023.

  • Tags

You can share this post!

FASIHI SIMULIZI: Soma kisa kifuatacho kisha ujibu maswali

DPP aomba korti idumishe adhabu dhidi ya Oswago

T L