VIONGOZI wa Kenya Kwanza wamemkashifu kiongozi wa Azimio la Umoja One Kenya, Raila Odinga kwa kutishia kuagiza wafuasi wake kurudia maandamano iwapo mazungumzo ya pande mbili yanayoendelea yatafeli.
Viongozi wa muungano tawala wakiongozwa na Rais William Ruto wamemtaja Bw Odinga kama adui wa amani anayetaka kutumia ghasia kuendeleza ajenda zake za kisiasa huku maelfu ya Wakenya wakifariki na kupoteza mali.
Rais Ruto alisema serikali yake inalenga kuinua umoja kati ya Wakenya na kutangaza kuwa yeyote anayechochea umma dhidi ya azima yake ni adui wa wengi.
“Sitakubali maandamano tena. Wamezoea kutumia ghasia kuharibu mali na uthabiti wa uchumi . Hayo hayatakubaliwa na hata ni kinyume cha sheria,” akasema Dkt Ruto akiwa Bungoma katika siku yake ya pili ya ziara ya siku nne Magharibi mwa Kenya.
Akiwa Kajiado, Jumamosi, Bw Odinga alisema upinzani utarudia maandamano mazungumzo yakifeli.
Bw Odinga alimuonya Naibu Rais Rigathi Gachagua kwa kupinga mazungumzo.