• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 7:50 PM
Shule zakosa maji ya kupikia watoto

Shule zakosa maji ya kupikia watoto

Na WAANDISHI WETU

WALIMU katika baadhi ya shule za Kaunti ya Tana River, wamelazimika kuwapa watoto chakula kibichi ili wakajipikie nyumbani kwa vile hakuna maji ya kupika.

Imebainika kuwa, watu zaidi ya 60,000 wako hatarini kuathirika na njaa katika maeneo tofauti ya kaunti hiyo.Mratibu wa Mamlaka ya Kitaifa ya Kudhibiti athari za Ukame, tawi la Tana River, Bw Abdi Musa, alisema Kaunti Ndogo za Bura, Tana Delta na Tana River ndizo zina mahitaji zaidi.

Katika maeneo ya Kone na Asa yaliyo Tana Delta, imeripotiwa zaidi ya familia 200 zilihama makwao ili kutafuta chakula na maji kwa kuwa mvua haijanyesha katika baadhi ya maeneo hayo tangu mwaka uliopita.

“Shuleni kuna chakula kilichohifadhiwa, lakini tatizo ni jinsi ya kupika chakula hicho. Hakuna maji. Masomo yanaathirika,” akasema.

Wanafunzi waliotegemea chakula cha shuleni sasa hupewa chakula kibichi ambacho watahitajika kupikiwa na wazazi wao, kisha wabebe wanapoenda shuleni ili wale wakati wa mchana.

Baadhi ya familia sasa hutegemea chakula hicho hicho ambacho watoto hupewa shuleni. Waziri wa Kilimo, Bw Peter Munya alisema baraza la mawaziri litakutana wiki ijayo kujadili baa la njaa linalokumba zaidi ya watu milioni katika takriban kaunti 12 nchini, ili kuamua njia mwafaka za kuepusha maafa.

Kati ya mikakati ambayo serikali inazingatia, ni kununua mifugo kutoka kwa wafugaji ili kuwaepushia hasara kwa sababu mifugo wameanza kufa katika baadhi ya maeneo.

Vile vile, serikali inatarajiwa kuamua jinsi ya kufikia idadi kubwa zaidi ya wananchi wenye mahitaji na kuwapa pesa za kununua chakula.

“Tumekuwa tukitathmini hali ilivyo. Tuna kamati katika la baraza la mawaziri ambayo inahusika na masuala ya ukame na baa la njaa. Kamati hiyo inaweka mikakati ya haraka ya kusaidia waathiriwa,” alisema Bw Munya.

Ijapokuwa Bw Munya alizidi kusema wizara yake imeanza kuandaa wakulima kwa msimu wa mvua, utabiri wa hali ya hewa uliotolewa mapema wiki hii, ulionyesha kuwa bado kutakuwa na uhaba wa mvua msimu huu.

Magavana wa kaunti za Kaskazini Mashariki, walimtaka Rais Uhuru Kenyatta, atangaze hali inayoshuhudiwa kuwa janga la kitaifa.

“Hali imeharibika zaidi kwa sababu ya uvamizi wa nzige ulioshuhudiwa awali ambapo mimea iliharibiwa. Sasa kuna ukame ambao tayari umeonyesha athari zake katika maeneo kama vile Kutolo na Mandera Magharibi, na vile vile sehemu za Kaunti ya Wajir,” akasema Gavana wa Mandera, Bw Ali Roba.

Kando na kuililia serikali kuu, walishauri kaunti zinazokumbwa na njaa kuhakikisha kuna bajeti ya kusaidia wananchi, kando na zile za kupambana na janga la corona.Katika Kaunti ya Lamu, Kamishna Irungu Macharia alisema takriban Sh100 milioni zinahitajika kwa dharura ili kusaidia waathiriwa wa njaa.

Mkurugenzi wa NDMA, Kaunti ya Lamu, Bw Mohamed Dahir, alisema wafugaji kutoka kaunti jirani za Tana River na Garissa, tayari wamefurika Lamu, na kusababisha hofu ya migogoro kuhusu sehemu za malisho.

Ripoti za Stephen Oduor, Winnie Atieno, Farhiya Hussein na Kalume Kazungu

You can share this post!

Sheria njiani kupunguza walinzi wa DP hadi 30

Wakenya kusisimua Diamond League Omanyala akishirikishwa...