Na JARED NYATAYA
Vijana anaodai kutapeliwa pesa zao kwa ahadi ya kupelekwa nchini Qatar kufanya kazi wakati wa Kombe la Dunia walisimamisha shughuli kwa muda mjini Eldoret leo, Agosti 28, 2023 baada ya kufanya maandamano wakitaka warudishiwe pesa zao na wahusika watiwe mbaroni.
Vijana hao ambao walibeba mabango ya kukemea ulaghai waliosema wamepitia chini ya mikono ya shirika la First Choice Recruitment Agency linalofanya shughuli ya kusajili wanaotafuta kazi ughaibuni walikemea kupewa hundi walizosema zimegeuka hewa.
Wiki jana, waathiriwa wa utapeli huu walipandwa na jazba walipokuwa wanahadithia Tume ya Bunge kuhusu Ajira jinsi shirika hilo linalohusishwa na mfanyabiashara Judy Chepchirchir liliwalaghai mamilioni ya pesa.
Ni tukio lililofanya Kamati hiyo kumuita Bi Chepchirchir kufika mbele yao kujieleza, ingawa alikosa kufanya hivyo na kutuma mwakilishi wake.
Katika maandamano hayo ya adhuhuri, polisi waliwasili muda mchache baadaye na kuwatawanya wakiwataka kupeleka malalamishi yao katika afisi husika za serikali.