• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 4:42 PM
Wakazi wa Pwani kuhamishiwa bara

Wakazi wa Pwani kuhamishiwa bara

Na MUSA IDDI

WAKAZI wa kaunti za Pwani ya Kenya zinazopakana na Bahari Hindi watahamishiwa bara, baada ya kugunduliwa kwa kiasi kikubwa zaidi cha dhahabu kuwahi kupatikana duniani.

Kulingana na kampuni ya Kenya Coast Gold Exploration and Mining Inc, kaunti ambazo zaidi ya wakazi wake asilimia 80 watahamishwa ni Kilifi, Kwale, Lamu na Mombasa.

Stakabadhi ambazo mwandishi wetu alisoma zinaonyesha kuwa wakazi hao watahamishiwa kaunti za Turkana, Marsabit, Mandera, Wajir, Garissa, Kiambu, Nyeri na Kisii

“Tutahakikisha kuwa wakazi wamelipwa fidia kwa kupoteza ardhi na mali yao nyingine ili waweze kutoa nafasi ya uchimbaji wa madini hayo. Mahali wataenda tutawajengea hospitali, shule, kuwawekea stima, maji na barabara za kisasa,” alisema mkuu wa kampuni hiyo, Niklas Saizler.

“Tumekuwa tukifanya utafiti eneo la Pwani ya Kenya kwa muda mrefu na sasa tumethibitisha kuna dhahabu nyingi na ya thamani kubwa,” akasema Saizler.

“Kiasi kikubwa zaidi kinapatikana Lamu chini ya bahari. Dhahabu hiyo ni ya ubora wa juu kuliko nyingine yoyote duniani,” akaongeza.

Alisema mpango huo wa kuhamisha wakazi utaanza kutekelezwa baada ya kushauriana na viongozi wa eneo hilo na kukubaliana kuhusu fidia inayopasa kulipwa wakazi.

Hata hivyo, baadhi ya wakazi waliozungumza na wanahabari walisema hawatakubali kamwe kuondoka Pwani hata kama watalipwa mamilioni ya pesa.

“Sitotoka hapa mie. Hii ni dhuluma kubwa. Huwezi ukatuhamishia bara eti kwamba unataka kuchimba dhahabu katika mashamba yetu. Mungu alikuwa na sababu alipotupatia makao hapa! Hata nikifa, mwili wangu hautatoka Pwani,” akasema Juma Charo, mkazi wa eneo la Shimo la Kale.

Viongozi wa makundi ya kijamii pia walipinga pendekezo hilo.

“Hao watu wanaota mchana. Hakuna vile utahamisha mamilioni ya wakazi kwa sababu unataka kuiba raslimali zao. Tutapigana nao hadi mwisho,” akaeleza Sheriff Karim kutoka Lamu.

You can share this post!

Daraja la Liwatoni lazidisha hatari ya kuenea kwa corona

Upanuzi wa uwanja wa ndege wa Manda waanza