NA WINNIE ATIENO
WAWEKEZAJI katika sekta ya utalii eneo la Pwani, wameisihi serikali kutatua mgomo wa marubani ambao wamedai umelemaza biashara zao.
Walieleza kuwa, watalii wengi wameshindwa kuzuru eneo la Pwani kwa mapumziko kufuatia ukosefu wa usafiri baada ya marubani wa kampuni ya Kenya Airways kususia kazi.
Wamemtaka Rais William Ruto kutatua migogoro katika shirika hilo la usafiri kabla ya Desemba, ambao ni msimu wa watalii kufurika katika Pwani ya Kenya.
Wawekezaji hao wamehoji kuwa, mgomo huo umetokea wakati wengi wao walikuwa wakijiandaa kuelekea jijini London, kwa maonyesho ya 43 ya kitalii ya mji huo (WTA London).
Washikadau hao walipaswa kuelekea jijini humo, kuvumisha bidhaa zao kama njia ya kutafuta soko.
“Mgomo huu umetokea wakati mbovu sana. Inatupa wasiwasi, kwani marubani wetu wamegoma,” alisema Mkurugenzi Mkuu wa Muungano wa wafanyikazi wa Hoteli na Wapishi, Sam Ikwaye.
Bw Ikwaye alimuomba waziri wa uchukuzi na miundomsingi Bw Kipchumba Murkomen, kusuluhisha mizozo inayowafanya marubani hao kugoma.
KQ imelazimika kuhamishia wateja wake katika mashirika mengine kama vile Jambo Jet, ambayo yamekuwa mstari wa mbele kuwaokoa wasafiri ambao safari zao zilikuwa zimesitishwa.
Mwenyekiti wa utalii katika ukanda wa Pwani (KCTA) Bw Victor Shitakha, alieleza kuwa mgomo huo umefanya watalii wengi kuahirisha safari zao.
Subscribe our newsletter to stay updated