NA MAUREEN ONGALA
IDARA ya Mahakama inalenga kusuluhisha takriban kesi 50 za ubakaji katika mwezi wa Novemba, katika mahakama ya Mariakani eneo bunge la Kaloleni.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mwezi wa kushughulikia kesi za watoto, Hakimu Mkuu wa Mahakama ya Mariakani, Bw Stephen Kalaingi, alidokeza kuwa kuna zaidi ya kesi 100 zinazohusu watoto ambazo hazijasuluhishwa.
“Tumechagua kesi ambazo zimekaa sana. Tutaanza na kesi zilizowasilishwa mahakamani mnamo 2020 kurudi nyuma. Tutazipa kipaumbele kesi hizo ili watoto wapate haki zao,” akasema.
Kulingana na Bw Kalaingi, visa vya ubakaji vinavyohusisha watu wazima vimeongezeka katika siku za hivi karibuni, na kusisitiza umuhimu wa kukabiliana na kesi hizo kwa uharaka.