Na RICHARD MUNGUTI
WATALAAM wawili wa kupima magonjwa walishtakiwa Jumanne kwa kujitengenezea cheti feki za taaluma hiyo.
John Mbathi Kariuki na Virginia Wanjiku Mwangi walishtakiwa katika mahakama ya Milimani Nairobi.Wote wawili walikabiliwa na mashtaka tisa ya ufisadi.
Kiongozi wa mashtaka Bw Abel Omariba alimweleza hakimu mwandamizi Bw David Ndungi kwamba wawili hao walitiwa nguvuni katika hospitali kuu ya Kenyatta (KNH) walipoenda kuomba kazi.Wote wawili Mbathi na Wanjiku walimkabidhi afisa wa usiamizi wa wafanyakazi Bw Patrick Opisa vyeti vyao feki kabla ya njama zao kuguduliwa.
Mahakama ilifahamishwa wawili hao walijifanya wao ni wataalam katika masuala ya maabara za kupima magonjwa waliosajiliwa na kupewa vyeti na bodi ya KMLTTB (kenya medical laboratory technology and technicians board).
Wawili hao walimkabidi Bw Opisa vyeti hivyo feki mnamo Machi 9 2020 katika Hospitali Kuu ya Kenyatta (KNH).Washtakiwa walikanusha mashtaka na kuomba waachiliwe kwa dhamana.Kila mmoja aliachiliwa kwa dhamana ya Sh500,000 hadi kesi itakaposikizwa na kuamuliwa.