• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 10:50 AM
Zizi la Man United laungua nyota mwingine akipatwa na kashfa ya mapenzi

Zizi la Man United laungua nyota mwingine akipatwa na kashfa ya mapenzi

CHRIS ADUNGO na MASHIRIKA

FOWADI wa Manchester United na timu ya taifa ya Brazil, Antony dos Santos, anachunguzwa na polisi nchini Uingereza na jijini Sao Paulo baada ya mchumba wake wa zamani, Gabriela Cavallin, kutoa madai mapya dhidi yake.

Mwanzoni mwa wiki hii, Gabriela alidai kuwa Antony, 23, alimtishia maisha akiwa mjamzito, akaharibu pandikizi kwenye titi lake, akamkata kidole kwa glasi na kutishia kumrusha nje ya gari lililokuwa likiendeshwa kwa kasi.

Hata hivyo, nyota huyo wa zamani wa Ajax ya Uholanzi amepinga vikali shutuma hizo za hivi punde kutoka kwa Gabriela japo ameungama kuwa uhusiano wao wa zamani kimapenzi ulikuwa na “misukosuko.”

“Ingawa uhusiano wetu ulikuwa na pandashuka tele, hakukuwa na dhuluma za kimwili dhidi ya Gabriela. Hivyo, madai yake si ya kweli,” akasema Antony.
Licha ya imani yake kwamba uchunguzi mpya wa polisi ungefichua kwamba hana hatia yoyote, Antony alijikuta akitemwa na timu yake ya taifa kwa minajili ya mechi zijazo za kufuzu kwa fainali za Kombe la Dunia za 2026 dhidi ya Bolivia na Peru.

Katika muda wa saa 24 zilizofuata baada ya Gabriela kuzua madai hayo dhidi ya Antony mnamo Jumatatu wiki hii, kulikuwa na ongezeko la shinikizo kutoka kwa mashirika ya kukabiliana na unyanyasaji wa kijinsia na dhuluma za kimapenzi zikitaka Man-United kuchukua hatua kali za kinidhamu.

Shirika moja ni la Countdown linalosimamiwa na shabiki sugu wa muda mrefu wa Man-United, Rachel Riley, ambaye pia alikashifu vikali tukio la mvamizi Mason Greenwood kuondolewa mashtaka licha ya madai mazito ya ubakaji yaliyotolewa dhidi yake mnamo 2021.

Rachel alitaja matukio yanayodaiwa kufanywa na Antony kuwa ya “kuchukiza mno” na amewataka wataalamu kuhusishwa kikamilifu katika juhudi za kuhamasisha wanasoka dhidi ya dhuluma za kimapenzi.

Wakati uo huo, Mkurugenzi wa Muungano wa Kukabiliana na Unyanyasaji dhidi ya Wanawake, Andrea Simon, ameambia Man-United kwamba “ulimwengu mzima unatazama jinsi wanavyoshughulikia masuala ya dhuluma za kimapenzi dhidi ya wanasoka wao.”

Hata hivyo, mabingwa hao mara 20 wa Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) wametoa taarifa wakisisitiza kwamba wanalichukulia suala hilo kwa uzito na uzingativu mkubwa.

Lakini wanasubiri uchunguzi wa polisi katika pande zote za Atlantic kukamilika kabla ya kuamua kuhusiana na hatua watakazozichukua.

  • Tags

You can share this post!

TUONGEE KIUME: Kutuma nauli na utapeli mwingine wa baadhi...

Utafiti wabaini ARVs hutumika kunenepesha kuku, nguruwe

T L