• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 7:55 AM
Turkana kifua mbele katika usajili wa kura

Turkana kifua mbele katika usajili wa kura

Na KENYA NEWS AGENCY

KAUNTI ya Turkana imeorodheshwa ya kwanza nchini katika shughuli inayoendelea ya usajili wa wapigakura.

Kulingana na ripoti ya hivi punde ambayo Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) ilitoa mnamo Oktoba 16, 2021, kaunti ya Turkana imesajili wapigakura wapya 10,539 kutoka kwa wapigakura 62,500 waliolengwa.

Hii ni sawa na kiwango cha ufanisi usajili cha asilimia 16.9

Meneja wa Uchaguzi katika kaunti ya Turkana George Oyugi alisema licha ya kwamba tume hiyo imefikia idadi hiyo ya usajili, uhamasisho duni na ukosefu wa usaidizi kutoka kwa viongozi, utaathiri kuafikiwa kwa lengo hilo.

“Nawaomba viongozi kujitokeza wawahimize watu wajitokeze ili tuweze kuwasajili wote waliosalia ndani ya wiki mbili zilizosalia. Watu wasisubiri hadi dakika za mwisho,” akasema Bw Oyugi.

Meneja huyo wa Uchaguzi pia alisema idadi kubwa ya watu hawana vitambulisho vya kitaifa licha ya kwamba baadhi ya stakabadhi hizo zimetengenezwa.

Bw Oyugi, alitoa wito kwa Shirika la Usajili wa Watu (NRB) katika kaunti ya Turkana liwasilishe vitambulisho kwa wenyewe ili waweze kujisajili kuwa wapigakura.

Alitoa wito kwa viongozi wa serikali ya Turkana kusaidia IEBC kufikia lengo la usajili wa wapigakura.

Bw Oyugi alisema serikali zingine za kaunti zinashirikiana na IEBC kwa kuwasafirisha watu katika vituo vya usajili pamoja na kutoa uhamasisho kuhusu zoezi hilo.

“Viongozi wa kaunti ya Turkana wanafaa kuiga mfano wa kaunti hizi. Inavunja moyo kwamba viongozi wa hapa hawajitokeza kupiga jeki shughuli hii,” akalalamika afisa huyo.

You can share this post!

Wanaotaka ugavana wamsuta Wetang’ula kupendekeza...

Mshukiwa wa mauaji ya Tirop kuzuiliwa siku 20

T L