• Nairobi
  • Last Updated May 18th, 2024 8:55 AM
Mshukiwa wa mauaji ya Tirop kuzuiliwa siku 20

Mshukiwa wa mauaji ya Tirop kuzuiliwa siku 20

Na TITUS OMINDE

MSHUKIWA mkuu katika mauaji ya mwanariadha chipukizi, Agnes Tirop atazuiliwa kwa siku 20 katika kituo cha polisi cha Eldoret baada ya mahakama kukubali ombi la kumzuilia ambalo liwasilishwa katika mahakama ya Iten na maafisa wa jinai.

Hakimu mkuu mwandamizi wa Iten, Charles Kutwa alitoa agizo hilo baada ya mshukiwa huyo, Ibrahim Rotich kufikishwa mahakamani mjini Iten, Jumatatu.

Rotich anashukiwa kumuua Bi Tirop Jumatano wiki jana.

Mshukiwa huyo alifikishwa kortini mwendo wa saa tatu unusu asubuhi chini ya ulinzi mkali wa zaidi ya maafisa 10 wa polisi, ambao walikuwa wamejihami.

Kulitokea kizaazaaa katika lango la mahakama hiyo, pale umati wa wananchi wenye ghadhabu ulipotaka kuruhusiwa ndani ya mahakama ili kujionea mshukiwa huyo.

Maafisa wa polisi walilazimika kuzuia raia kuingia kortini humo, ila waliruhusu tu mawakili na wanahabari kwa kuhofia usalama wa mshukiwa.

Hakimu Kutwa aliamuru mshukiwa azuiliwe katika kituo cha polisi cha Eldoret kwa siku 20, ili kufanikisha uchunguzi kabla ya kusomewa mashtaka husika.

Vile vile mahakama iliamuru mshukiwa kufikishwa hospitalini ili kufanyiwa uchunguzi wa kiakili, kubaini iwapo atafunguliwa mashtaka ya muaji.

“Kwa kuwa hili ni suala linalohusu kesi ya mauaji, ninaelekeza kwamba litajwe katika Mahakama Kuu ya Eldoret hapo Novemba 9 kwa maagizo zaidi,” aliamuru hakimu.

Agizo hili lilitokana na ombi la Mkurugenzi Mwandamizi wa Mashtaka ya Umma, Judith Ayuma, ambaye aliambia mahakama kuwa uchunguzi wa polisi bado haujakamilika.

Polisi wanalenga kuwakamata washukiwa zaidi kuhusiana na mauaji hayo.Kwa mujibu wa polis, mshukiwa huyo mkuu katika mauaji hayo, alikamatwa Alhamisi katika eneo la Changamwe Kaunti ya Mombasa, wakati akijaribu kukimbilia nchi jirani.

You can share this post!

Turkana kifua mbele katika usajili wa kura

Bodi yasaka chanzo cha jengo kuporomoka

T L