NA FARHIYA HUSSEIN
SERIKALI ya Kaunti ya Mombasa imeitaka Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kutoa ripoti iliyo na maelezo ya kina kuhusu madai ya unyakuzi wa mashamba katika kaunti hiyo.
Katika taarifa yake kwa umma hivi majuzi, tume ya EACC iliweka bayana kwamba Kaunti ya Mombasa inaongoza kwa visa vya unyakuzi wa ardhi, tume hiyo ikisema inakagua kesi zote za ardhi ambazo tayari zimewasilishwa mahakamani ili kuwaandama wanyakuzi hao.
Aidha, serikali ya kaunti ya Mombasa imesema haipingi ripoti ilitolewa na EACC wakitaka maelezo zaidi kutolewa kwenye ripoti hiyo.
Waziri wa Ardhi katika Kaunti ya Mombasa Bw Hussein Mohammed alisema serikali hiyo iko tayari kufanya kazi na EACC ili kusitisha unyakuzi wa ardhi wa kila uchao, huku akiitaka tume hiyo kuisaidia serikali ya kaunti hiyo kuwatambua wanyakuzi sugu wa ardhi.
Akizungumza jijini Mombasa, waziri Mohammed amehoji kwamba sheria haitamsaza yeyote aliyenyakua ardhi ya umma na kuwahangaisha wakazi, akiwataka wale wanaomiliki vyeti bandia walivyotumia kuwafurusha wenyeji kusalimisha vipande hivyo ardhi hizo.
Bw Mohammed aliongezea ya kuwa Serikali ya Kaunti ya Mombasa inaendeleza jitihada za kuhakikisha kuna maafikiano kati ya wamiliki halisi wa ardhi na maskwota ili kuzima matukio ya watu kufurushwa kwenye ardhi walizoishi kwa miaka mingi.