Na Winnie Onyando
MUUNGANO wa Azimio la Umoja One Kenya umetangaza kuwa utaendelea na maandamano Alhamisi Mei 4, 2023.
Akihutubia wanahabari Jumanne, kiongozi wa chama cha Narc-Kenya Martha Karua alisema muungano huo utaendelea na maandamano ya kuipinga serikali ya Kenya Kwanza siku ya Alhamisi.
“Tutaendelea kuandamana. Jumatano tunapumzika ili kupanga jinsi tutakavyoendeleza maandamano Alhamisi,” akasema Bi Karua.
Muungano huo pia umedai kuwa serikali tawala ilipanga kuvuruga maandamano ya Jumanne Mei 2, 2023.
“Tulipokea taarifa kuwa serikali ya Kenya Kwanza ilipanga kuvuruga maandamano yetu ili kutupaka tope,” akaongeza Bi Karua.