NA MAUREEN ONGALA
HAKIMU Mwandamizi Mkuu wa Kilifi Justus Kituku amewaruhusu polisi kumzuilia mshukiwa Diana Naliaka almaarufu Sarah Nekesa Barasa kwa siku 14 katika kituo cha polisi cha Kilifi.
Kiongozi wa mashtaka Bi Winnie Atieno Otieno ameiomba mahakama muda zaidi wa kumzuilia Naliaka, ambaye ndiye mshukiwa mkuu wa mauaji ya Afisa Mkuu wa Uchumi wa Baharini katika Kaunti ya Kilifi marehemu Rahab Karisa.
“Nimesikiliza ombi la kiongozi wa mashtaka kuomba muda zaidi kumzuilia mshukiwa ili kukamilisha uchunguzi wao. Sina pingamizi kwa hilo nikizingatia uzito wa kesi hiyo,” akasema hakimu Kituku.
Rahab aliuawa kwa kudungwa kisu nyumbani mnamo Alhamisi, Julai 20, 2023.
Inadaiwa mtafaruku ulitokea baada ya yeye kurejea nchini kutoka Italia alikohudhuria mkutano muhimu wa kimataifa na akapata pesa zake kiasi fulani zilikuwa zimepotea nyumbani.
Mshukiwa Naliaka alikamatwa katika eneo la Misikhu akitembea kwa miguu akiwa na lengo la kuingia nchini Uganda. Afisa wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai katika Kaunti ya Kilifi Bw David Siele alithibitisha kwamba mshukiwa alikamatwa mnamo Jumanne saa kumi alfajiri akipanga kutorokea katika taifa jirani.
Kesi dhidi ya mshukiwa itatajwa Agosti 17, 2023.